WAUGUZI na Wakunga nchini wametakiwa kuepuka kutoa lugha zisizofaa kwa wagonjwa kwani kufanya hivyo ni kinyume cha maadili na miiko ya taaluma hiyo.
Mkurugenzi wa huduma za Uuguzi na Ukunga kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ziada Sellah ameyasema hay oleo jijini Dar es Salaam wakati wa kikao kazi na wauguzi na wakunga wa mkoa huo.
Mkurungezi huyo amesema kumekuwa na tabia chafu ya baadhi ya wauguzi na wakunga kutoa lugha zisizofaa kwa wagonjwa jambo linaloharibu taswira ya taaluma hiyo.
Aidha Ziada ametoa wito kwa wauguzi kujiendeleza kielimu ili waweze kujiongezea maarifa katika utaalamu wao wa kutoa huduma bora na zenye tija kwa wagonjwa.
Pia amewaasa watumishi wa sekta hiyo ya afya kufanya kazi kwa umoja na mshikamano wakizingatia suala la uwazi.
Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Dr. Rashid Mfaume ametoa wito kwa wauguzi kuheshimiana na kuthaminiana katika mazingira ya kazi.