KUANZIA Februari 16, mwaka huu vituo vya afya vya umma vinavyotibu wagonjwa wa covid-19 vitaanza kutumia bima ya afya kwa ajili ya kutibu wagonjwa hao.
Kwa mujibu wa waraka uliotolewa na Waziri wa Nchi wa Huduma ya Afya ya Msingi, Dk Tharcisse Mpunga kwenda hospitali za umma nchini kote, wizara hiyo imeamua kujumuisha ugonjwa wa covid-19 katika utaratibu wa bima ya afya.
Hii itajumuisha huduma za nyumbani na matibabu katika vituo vya afya, hospitali za wilaya na rufaa.
Hapo awali, gharama ya matibabu ya covid-19 katika vituo vya umma zilitolewa na serikali kwa kutoa matibabu bure.
Mkuu wa Idara ya Huduma za Kliniki na Afya ya Umma katika Wizara ya Afya, Dk Corneille Ntihabose alisema matibabu ya ugonjwa huo yanahusisha gharama za usafirishaji wagonjwa, hewa ya oksijeni, dawa, tiba na ushauri, huku upimaji katika vituo vya umma ukibaki kuwa bure.
“Hakuna mtu atakayekosa matibabu kwa kukosa bima ya afya kwani kuna njia nyingine kwa wagonjwa wasio na bima kupata matibabu kupitia ushirikiano na wizara au serikali za mitaa na wilaya,” alisema.
Dk Corneille Ntihabose alisema aina zote za bima, miradi ya binafsi ya bima ya afya inayojulikana kama Mutuelle de santé pamoja na bima ya Rama ya Bodi ya Hifadhi ya Jamii ya Rwanda itakubaliwa katika vituo vya afya vya umma nchini.