Dodoma. Serikali imeanza mchakato wa mabadiliko ya sheria ili kuwezesha upimaji wa kushusha umri wa upimaji wa virusi vya ugonjwa wa ukimwi (VVU) kutoka miaka 18 hadi 15.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Dk Faustine Ndungulile amesema hayo bungeni leo wakati alipokuwa akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu na Mfuko wa Bunge kwa mwaka wa fedha 2019/2020.
Amesema katika kufikia malengo ya asilimia 90 katika kupima, matibabu, kufubaza maambukizi mapya ya ugonjwa wa ukimwi, Serikali imeona kuna changamoto katika kundi la vijana na wanaume.
Amesema kutokana na hilo wameamua kuja na mabadiliko ya sheria ili kuruhusu upimaji binafsi na kushusha umri wa upimaji wa virusi vya ukimwi kufikia 15
Amesema mabadiliko hayo yako katika ngazi mbalimbali za taratibu za kiserikali na zitakapokamilika zitapelekwa bungeni.
Dk Ndungulile amesema kumekuwa kutokana na ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza wanajipanga upya katika maeneo mbalimbali.
Amesema Serikali iko katika hatua za mwisho kuanzisha mpango wa taifa wa magonjwa yasiyoambukiza ili kuwapo kwa utaratibu mzuri wa kudhibiti magonjwa hayo.