Dar es Salaam. Wakati waliokufa kutokana na ajali ya moto mjini Morogoro ikifikia 100 hadi leo mchana Jumatano Agosti 21, 2019, madaktari wamesema sababu ya vifo hivyo ni kuungua kwa kiasi kikubwa na kuvuta moshi.
Ajali hiyo ilitokea Agosti 10, 2019 katika mtaa wa Itingi, Msamvu barabara ya Morogoro-Dar es Salaam baada ya lori la mafuta kupinduka na kuwaka moto muda mfupi baada ya watu kuanza kuchota mafuta.
Tangu siku hiyo hadi leo watu 100 wamekufa huku wengine 15 wakiendelea na matibabu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).
Hayo yameelezwa leo na madaktari bingwa wa upasuaji wanaowatibia majeruhi hao waliohamishiwa hapo kutoka Hospitali ya Mkoa wa Morogoro. Majeruhi walioletwa MNH kutoka Morogoro walikuwa 47 na sasa wamebaki 15 baada ya wengine 32 kufariki.
Dk Lauren Rwanyuma amesema majeruhi waliopelekwa MNH waliungua kwa zaidi ya asilimia 70 kiwango ambacho ni kikubwa zaidi kwa mwili kustahimili.
Amesema pamoja na kuungua kwa kiasi hicho majeruhi hao walivuta moshi mwingi ambao umeenda kuathiri sehemu za ndani za miili yao, ikiwemo figo na mapafu.
Habari zinazohusiana na hii
- Majeruhi 16 ajali ya lori Morogoro waendelea kuimarika, waanza mazoezi
- Majeruhi wawili ajali ya moto Morogoro wafariki, idadi yafikia 99
- RAS Morogoro azungumzia ujenzi wa mnala, uzio makaburi ya ajali ya lori
- Ajali ya moto Morogoro, vifo vyafikia 100
“Hata kama mtu ameungua kwa kiwango kikubwa kiasi gani jukumu la madaktari ni kuokoa maisha yake, wengi walikuja wameungua sana ila tulipambana na tunaendelea kupambana kuwanusuru waliobaki,” amesema Dk Rwanyuma.
Naye daktari bingwa wa upasuaji, Edwin Mrema amesema majeruhi hao pamoja na kuungua ngozi na kubaki wazi moshi waliovuta umeongeza hatari zaidi.