Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Utafiti waonyesha asilimia 24 wanaume wa Kinondoni wana tatizo la nguvu za kiume

58404 Pic+rijali

Sun, 19 May 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Utafiti uliofanyika katika Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam ulionyesha kuwa asilimia 24 ya wanaume wana tatizo la nguvu za kiume.

Mkuu wa Kitengo cha Utafiti katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, Dk Pedro Pallangyo anasema utafiti huo uliofanyika mwaka 2016 uliwachunguza wanaume 18,441 wote wakazi wa Dar es Salaam wilaya ya Kinondoni.

“Tulitumia dodoso moja linalotumika kimataifa linaloitwa IIEF5 ambalo ni maswali maalum yaliyoandaliwa na kuchunguzwa kama yanaweza kutoa majibu sahihi kwenye uchunguzi wa hilo tatizo, linatumika kimataifa na lilithibitishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO).

“Tuliowachunguza wastani wa umri wao ulikuwa miaka 47, karibu asilimia 60 ya wanaume wote walikuwa na uzito kupindukia, wanane kati ya 100 walikuwa na tatizo la kisukari na asilimia 61.5 walikuwa na shinikizo la juu la damu,” anasema Dk Pallangyo.

Anasema walitumia dodoso katika kuangalia kama kuna wenye shida ya nguvu za kiume. “Asilimia 24 karibu robo waliripoti kuwa na shida katika nguvu za kiume.”

Anasema wakati wakikusanya takwimu walihusisha sababu za upungufu huo na kubaini ni uzito mkubwa kupindukia, uvutaji wa sigara, unywaji pombe kupindukia, magonjwa hasa shinikizo la juu la damu na kisukari.

Pia Soma

“Kwa ujumla tuliweza kugundua kuwa wanaume waliokuwa na umri juu ya miaka 55, waliokuwa na historia ya uvutaji wa sigara, uzito kupindukia uwiano usio sawia kwenye BMI (uzito, urefu) juu ya 24.9, historia ya kisukari, shinikizo la damu waliripoti upungufu wa nguvu za kiume kwa kiwango cha juu zaidi ikilinganisha na wengine.”

Dk Pallangyo anasema visababishi vinashabihiana na kwamba mtu ambacho hana uwezo nacho ni umri pekee vingine vyote vinasababishwa na mtindo wa maisha.

Tiba sahihi

Licha ya changamoto kwa walio na tatizo hilo, daktari bingwa wa magonjwa ya mfumo wa mkojo kutoka Hospitali ta Taaluma na Tiba, Mloganzila (MAMC), Deogratius Mahenda anasema ipo suluhisho kwao ikiangaziwa na tiba sahihi baada ya vipimo vya maabara.

“Wanaume wengi akiona jogoo hapandi mtungi anakimbilia viagra, dawa za mitishamba halafu anabugia bila kupima. Hilo limewafanya wengi hata nguvu za awali kupotea kabisa.”

Anasema mara baada ya uchunguzi wa maabara, tatizo la upungufu wa nguvu za kiume huisha kabisa.

“Tunatoa vipimo vya aina mbalimbali lakini pia tiba ya saikolojia na wengi wanapata usaidizi kwani asilimia 90 ya kati ya wanaokuja ni tatizo la kisaikolojia.”

“Tunatoa pia dawa za kusisimua misuli kulingana na tatizo la mgonjwa zipo za vidonge na sindano sasa anashauriwa namna ya kutumia na sindano anaelekezwa namna ya kujichoma na inachomwa kwenye uume.”

Tiba lishe

Kuna makundi ya vyakula ambavyo wanaume anapaswa kula angali mdogo ili kulinda nguvu zake na vipo pia vya kuepukwa kama wanavyoshauri wataalamu wa lishe kutoka Hospitali ya Taaluma na Tiba Mloganzila, Theresia Thomas na Job Mbwilo.

Ofisa lishe, Theresia anasema ulaji wa protini, matunda na mlo kamili ndiyo dawa pekee ya kuhimili nguvu kwa mwanaume yeyote.

“Ulaji wa samaki, kuku na nyama kiasi husaidia kwani kuna chembechembe za acid ambazo husaidia utendaji kazi wa mwili na kuimarisha mishipa ya damu ila isizidi sana ikaleta mafuta mwilini, mazao ya samaki ikiwemo pweza, ngisi na mengineyo husaidia pia.”

Anayataja matunda kama tikiti maji na parachichi ambayo yana folic acid na nishati mwilini na berries ambazo huwezesha msukumo wa damu mwilini.

Anataja mbogamboga kama brocoli, spinachi na kabichi pamoja na nafaka za karanga, korosho ambazo huleta pia nishati mwilini pamoja na mbegu za maboga, bila kusahau viungo mbalimbali kama vitunguu swaumu, pilipili, kungu na mdalasini ambazo hufanya kazi ya kuamsha hisia.

Ofisa lishe, Job Mbwilo anaitaja chocolate nyeusi kuwa husaidia kuamsha hisia za mtu katika kufanya tendo na husaidia pia kusukuma damu kwenda maeneo husika, lakini kula vizuri na kushiba kabla ya tendo.

Dawa zilizopo

Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) imesema dawa ambazo zimesajiliwa na mamlaka hiyo baada ya kuchunguzwa na kuonekana zinafaa kutumiwa na binadamu ni aina mbili.

Msemaji wa TFDA, Gaudensia Simwaza alisema: “Kuna dawa aina mbalimbali zikiwemo Sildenafil na tadalafil zinazotoka nchi mbalimbali zilizochunguzwa na TFDA na kuonekana hazina sumu wala madhara kwa watumiaji, hizi zinapatikana katika maduka mbalimbali ya dawa za binadamu.”

Machi mwaka jana, Serikali ilitangaza rasmi kuzitambua aina tano za dawa za asili baada ya kuzikagua ikiwemo Ujana inayotibu nguvu za kiume, IH Moon, Coloidal Silver, Sudhi na Vatari.

Serikali kufanya utafiti

Naibu Waziri wa Afya, Dk Faustine Ndugulile amesema Serikali imeamua kufanya utafiti wa tatizo la ukosefu wa nguvu za kiume kwa wanaume kwa sababu kwa muda mrefu wamekuwa wakitafuta suluhisho kwa kificho na hivyo kukosa taarifa sahihi.

Alisema wizara kwa kushirikiana na Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR), inafanya utafiti wa afya ya uzazi kwa wanaume ili kubaini sababu ya ongezeko la upungufu wa nguvu za kiume ni kubwa kwa kiasi gani nchini.

Alisema kwa kipindi kirefu Serikali imekuwa ikitilia mkazo afya ya uzazi kwa wanawake na tafiti nyingi zimekuwa zikihusu upande huo mmoja. “Bado hatujafanya utafiti wa kina kujua tatizo hili ni kubwa kwa kiasi gani, suala hili ni gumu kulisemea kwa maana ukiangalia takwimu ya uzazi Tanzania kwa maana ya ongezeko la watu na idadi ya kinamama kukua unaona kabisa bado hatuna shida,” amesema.

Hata hivyo, alisema takwimu za kidunia sayansi inaonyesha kuwa wanaume wengi wana matatizo ya nguvu za kiume yanayosababishwa na mtindo wa maisha.

Dk Mahenda alisema vipandikizi hivyo vipo vya aina mbili kikiwemo kile kinachosimamisha uume muda wote na ambacho kinategemea msukumo ili kiweze kusimamisha.

Vipandikizi kuongeza nguvu

Wapo wasioweza kusimamisha kabisa au wale ambao kutokana na maradhi fulani, uume unaposimama hafiki kileleni na kubaki hivyo mpaka afanyiwe upasuaji mdogo.

Alisema vipandikizi hivyo wanaowekewa wanaweza kukaa navyo muda mrefu japokuwa wakati mwingine huhitaji kubadilishiwa.

“Huduma hii haitolewi sana hapa nchini na wanaofanyiwa si wale wa selimundu pekee ila na wengine ambao wanashindwa kabisa kusimamisha wanawekewa hivi vipandikizi.

“Ufanyaji kazi wake upo wa aina tofauti vipo uume unasimama muda wote na vingine unaweza kusimamisha na kuilaza kunakuwa na mechanism ambayo unaweza ku-pump na ukiachia inalala hivyo unasimamisha pale tu unapokuwa na uhitaji na hii pump yake huwekwa chini ya korodani,” anasaema daktari bingwa wa magonjwa ya mfumo wa mkojo kutoka Hospitali ta Taaluma na Tiba, Mloganzila (MAMC), Deogratius Mahenda.

Chanzo: mwananchi.co.tz