WIZARA ya Afya nchini Urusi imesajili dawa aina ya Leitragin ya kutibu na kuzuia maradhi ya nimonia yanayosababishwa na virusi vya corona.
Hayo yamebainishwa na Shirika la Matibabu na Baiolojia nchini humo lililosajiliwa na Wizara ya Afya ya Shirikisho la Urusi.
“Mei 25 mwaka huu, dawa ya Leitragin iliyotengenezwa na Shirika la Matibabu na Baiolojia la Shirikisho la Urusi imesajiliwa. Dawa hii mpya ni kwa ajili ya kutibu na kuzuia nimonia inayosababishwa na virusi vya corona,” lilisema baraza hilo.
Uzalishaji wa dawa hiyo kiwandani ulizinduliwa hivi karibuni.
Leitragin imetajwa kuwa dawa ya kwanza kutumika kwa ajili ya kuzuia na kupambana na matatizo yanayosababishwa na corona, ambayo imefanyiwa majaribio kwa wagonjwa 320 waliokuwa na dalili za kawaida za covid-19 na kubainika kuwa hakuna mgonjwa aliyekufa miongoni mwao, lakini pia hakuna aliyebadilika na kuwa na dalili kali za ugonjwa huo.
Imeelezwa kuwa wagonjwa waliopewa dawa hiyo walipona ndani ya siku nane ikilinganishwa na wale waliochukua siku 14 kupona baada ya kupewa matibabu ya kawaida.