Dar es Salaam. Jiji la Dar na viunga vyake litaanza kupuliziwa dawa ya viuadudu (Biolarvicides) ikiwemo mbu pevu ikiwa ni sehemu ya kupambana na ugonjwa wa homa ya dengue ambao hivi sasa ni tishio kwa wakazi wa Dar es Salaam.
Zoezi hili pia litafanyika katika mikoa ya Morogoro, Pwani na Tanga ambayo pia imeripotiwa kukumbwa na athari za ugonjwa huo.
Hayo yamezungumzwa leo Juni 2, 2019 wakati wa ziara maalum katika eneo la Jangwani jijini hapa iliyowakutanisha viongozi wa juu wa Waziri wa Afya wakiongozwa na Waziri, Ummy Mwalimu pamoja na viongozi wa mkoa wa Dar es Salaam.
Akizungumza baada ya ziara hiyo, Waziri Mwalimu ametoa maagizo kwa Katibu Tawala wa Mkoa (RAS) Aboubakar KunengeĀ kuhakikisha umwagiliaji dawa ya kuua viuadudu ikiwemo mbu pevu unaanza mara moja.
"Mvua zimeshamalizika sasa naagiza RAS muanze kupulizia dawa na zoezi hili halitazidi siku tano, mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro na Tanga. Pia naagiza wamiliki wa baa, mahoteli, makanisa, misikiti na nyumba moja moja kuchukua hatua ya upuliziaji wa dawa hii," amesema Mwalimu.
Naibu Waziri wa afya Dk Faustine Ndugulile amezungumzia suala la mkanganyiko uliopo katika vipimo vya ugunduzi wa homa hiyo (dengue)na kusema hivi sasa vipimo hivyo ni bure katika hospitali zote za umma.
Pia Soma
- Wakemia waaswa kuwa waadilifu
- Wakulima wa mkonge walilia uhaba wa wataalamu na soko
- UREMBO: Namna sahihi ya kuondoa vinyweleo
Kwa upande wake Kunenge amesema tayari wameanza maandalizi muda mrefu na kilichokuwa kikisubiriwa ilikuwa ni mashine za upuliziaji wa dawa hiyo.
Amesema watatumia vifaa vingi ikiwemo vya zimamoto na kwamba lazima wajiridhishe kwamba haviwezi kuwa na madhara kwa wananchi.