UONGOZI wa Hospitali ya Rufaa Bugando umewatoa hofu wagonjwa wa covid-19 na wananchi kwa ujumla, kwamba huduma ya hewa ya oksijeni inapatikana bila tatizo hospitalini hapo.
Hata hivyo, Kaimu Mkurugenzi wa hospitali hiyo, Dk Fabian Massaga, amesema kuna ongezeko kidogo la mahtaji ya hewa hiyo kutokana na uwepo wa wagonjwa hao.
Akitoa taarifa kwa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Robert Gabriel aliyetembelea hospitalini hiyo mwishoni mwa wiki, Dk Massaga alisema Hospitali ya Bugando ina mitambo miwili ya kuzalisha hewa ya oksijeni yenye uwezo wa kuzalisha asilimia 80 ya mahitaji.
“Tuna wagonjwa wa corona (covid-19) hapa na tunawapatia huduma stahiki bila ya matatizo," alisema.
Kwa upande wake, Gabriel aliwasistiza wananchi kuendelea kuchukua tahadhari ya ugonjwa huo kwani wimbi la tatu la virusi vya corona ni tishio.
Aliwataka wananchi kuendelea kufuata miongozo inayotolewa na wataalamu wa afya, hasa uvaaji barakoa na kutumia vitakasa mikono muda wote.
"Serikali yetu inapambana na vita hii ipasavyo na sisi wananchi tuiunge mkono kwa kuchukua tahadhari," alisema.