Hivi huwa unatafuna mbegu za ubuyu au hutafuni? Kama huwa unamung’unya tu bila kutafuna basi unakosa uhondo na faida inayopatikana katika tunda hilo.
Ubuyu ni tunda kama yalivyo matunda mengine, huimarisha kinga ya mwili na mifupa na hapa tunazungumzia ubuyu halisi (fresh) haujachanganywa rangi, ladha wala kitu kingine.
Ofisa lishe wa Mkoa wa Dodoma, Heriet Nyange anasema moja ya faida kubwa iliyopo katika ubuyu halisi una vitamini C nyingi zaidi kuliko matunda jamii ya machungwa na kizuri zaidi huongeza damu mwilini.
“Ubuyu una vitamini C nyingi, mara tano ya ile inayopatikana katika matunda jamii ya machungwa,” anasema Nyange.
Anasema mbali na vitamini C, ubuyu una vitamini A, E, B2 pamoja madini ya chuma, calcium, magnesium, potasium, folic, zinki na protini.
“ Tunda hili pia lina wanga, hivyo raha ya kula ubuyu utafune na mbegu zake na ule ubuyu ambao ni halisi, yaani haujawekwa rangi wala ladha.”
Pia Soma
- Aga Khan waanzisha kitengo cha dharura kutibu kiharusi
- Makosa 13 yanayoweza kukufunga kwenye uchaguzi serikali za mitaa
- Mwananchi yaiibua halmashauri Buchosa, yaahidi kujenga choo cha shule
Huondoa tatizo la kukosa choo kutokana na kwamba ubuyu una nyuzi nyuzi ambazo husaidia kurekebisha matatizo ya umeng’enywaji wa chakula.
“ Faida nyingine huondoa sumu na mafuta mwili.”
Nyange anabainisha kuwa hata majani ya ubuyu hutumika kama mboga kwa jamii ya Wagogo.
“ Huchuma majani ya ubuyu yale malaini na kuyapika, hivyo kupata mboga aina ya mlenda,” anasema.
Kuhusu watoto wenye umri wa miezi sita na kuendelea, mtaalamu huyo wa lishe anasema wanaweza kuchanganyiwa kidogo juisi ya ubuyu katika uji ili wapate vitamini C na virutubisho vingine.
Makala haya yameandikwa na mwandishi wa gazeti hili.