Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Ummy awatolea uvivu wasimamizi miradi ya afya

D6493ab788fdfa18d1981ebfdf6d63e1.jpeg Ummy awatolea uvivu wasimamizi miradi ya afya

Thu, 6 May 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Ummy Mwalimu ameonesha kutoridhishwa na usimamizi wa miradi ya afya katika Wilaya ya Chemba mkoani Dodoma.

Aidha alisema waliohusika kutafuna fedha katika miradi hiyo atawatafuta popote walipo na atawashughulikia.

Kauli hiyo aliitoa wakati akiwa katika ziara ya kukagua miradi ya maendeleo wilayani hapa ambapo alitembelea Hospitali ya Wilaya ya Chemba na Kituo cha Afya cha Hamai.

Waziri Ummy alisema ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Chemba haukusimamiwa vizuri na ndio maana baadhi ya majengo bado hayajakamilika kwa asilimia 100, huku akihoji ni kwa nini Sh milioni 250 zilirudishwa hazina wakati ujenzi haujakamilika.

“Lazima tukubali ujenzi haukusimamiwa vizuri hakukuwa na usimamizi mzuri wanaohusika na manunuzi, hawakusimamia

vizuri ndio maana Sh milioni 250 zikarudi lakini hapa hakuna hata wagonjwa kwa sababu huduma muhimu hakuna, mna wagonjwa 1,000 tu katika Hospitali ya Wilaya kuna shida,”alisema.

Waziri huyo alisema wote waliohusika na wizi katika miradi hiyo atahakikisha anawawajibisha hata kama wamehama katika halmashauri hiyo.

“Hii miradi imehujumiwa, watu wametanguliza maslahi binafsi najua Mhandisi aliondolewa ili watu wapige, ninayo majina wameharibu wamepelekwa kwingine sasa hata kama ulihamishwa mimi hili siliachi, tukithibitisha tunakupeleka mahakamani,”alisema.

Akiwa katika Kituo cha Afya cha Hamai, Waziri Ummy alipokelewa na wakazi wa vijiji vya Songolo na Hamai ambapo walidai huduma muhimu katika kituo hicho hazipatikani kama X-ray, dawa, maji, gari ya wagonjwa, wodi ya wanaume pamoja na uzio.

Katika hatua nyingine, Waziri Ummy amewataka wakuu wa mikoa, makatibu tawala mikoa, wakuu wa wilaya na wakurugenzi wa halmashauri kuendelea kuchapa kazi kama awali na sio kukaa kusubiria uteuzi.

“Hali inayoendelea kwa viongozi hawa haileti afya, wengine hawafanyi kazi eti wanasubiria mkeka, hamuoni kuwa mnaonea wananchi kupata haki yao ya msingi ya kuhudumiwa,” alihoji.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk Binilith Mahenge alisema atahakikisha maji yanapatikana katika hospitali ya wilaya na katika Kituo cha Afya cha Hamai.

Chanzo: www.habarileo.co.tz