Dar es Salaam. Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amewataka watoa huduma za dawa nchini kuzingatia weledi na maadili katika utoaji huduma hiyo.
Pia amewataka kuzingatia miiko ya taaluma yao ya ufamasia lengo likiwa kuhakikisha huduma zinazotolewa zinakuwa bora na salama.
Ummy ametoa wito huo leo wakati akizindua baraza jipya la famasi lenye jumla ya wajumbe saba.
Amesema dawa ni bidhaa nyeti ambazo kama zitatolewa bila kuzingatia sheria zinaweza kuleta madhara kwa wananchi.
"Kwa hiyo baraza hili lina jukumu kubwa kuhakikisha kuwa huduma hii inatolewa kwa kuzingatia misingi ya afya. Kwasababu tukisema turuhusu huduma hii itolewe kiholela hatuwezi kuipeleka sekta hii ndogo ya famasia mbele," amesema.
Kwa upende wake, msajili wa famasia nchini, Elizabeth Shekalage amesema baraza hilo litahakikisha lina imarisha na kudhibiti usimamizi wa sheria na kuchukua hatua stahiki kwa watakaokiuka.