Serikali imesema kiwango cha maambukizi ya Ukimwi Mkoa wa Tanga kimepungua kufikia asilimia 2.9% ukilinganisha na asilimia 4.4% ya kitaifa.
Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema hayo Februari 23, 2024 alipopokea na kukabidhi vitendea kazi vya Sh milioni 800 kutoka kwa wadau wa sekta ya afya CDC kupitia THPS kwa ajili ya mapambano dhidi ya Ukimwi na Kifua Kikuu mkoani humo.
“Hata kama maambukizi yamepungua katika mkoa wetu, tusibweteke, tunaomba kila mmoja wetu apime virusi vya Ukimwi ili kujua hali ya maambukizi na ukigundulika una maambukizi tunakuanzishia dawa ili uendelee kuishi maisha mazuri”. Amesema Ummy.
Ummy ameeleza katika kila watu 100 wanaotumia dawa za kufubaza makali ya Ukimwi katika Mkoa wa Tanga, watu 98 wamefubaza makali ya virusi na kupelekea kupunguza nafasi ya kumuambukiza mwengine.