Wanafunzi 150 wa udaktari kutoka Chuo Kikuu cha Tiba, Sayansi na Teknolojia (UMST) cha Khartoum nchini Sudan wamehamishiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) ili kukamilisha mwaka wao wa mwisho wa masomo.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa kuwakaribisha wanafunzi hao, Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Prof. Mohamed Janabi amesema kuwa hali ya mapigano ya wenyewe kwa wenyewe yanayoendelea nchini Sudan imesababisha kufungwa kwa vyuo na baadhi ya shughuli kusimama hivyo watalamu hao kushindwa kuendelea na ratiba yao ya masomo ya kawaida.
“Wanafunzi hawa wapo mwaka wa tano wa shahada ya kwanza ya utabibu, ambapo katika mwaka huo, mafunzo hufanyika kwa vitendo zaidi, hivyo madaktari hawa wanafunzi watafanya mzunguko (Rotation) katika idara mbalimbali” amesema Prof. Janabi
Amebainisha kuwa MNH itatoa fursa kwa wataalamu hao kujifunza kama ambavyo inatoa kwa wataalamu wengine wa ndani na nje ya nchi na hata baada ya kumaliza masomo kama watapenda kufanya mafunzo tarajali (Intenship).
Mapigano kati ya jeshi na wanamgambo nchini Sudan yamesababisha vifo, kujeruhi, kuharibu mahospitali na kusabisha shule na vyuo kufungwa.
Mamia ya wanafunzi wa mataifa mbalimbali walikimbia mgogoro na kurudi katika nchi zao.