Serikali kupitia Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto imekanusha kuhusika na masharti ya chanjo ya Corona kwa wasafiri wanaokwenda nje ya nchi.
Kupitia taarifa iliyotolewa na Kaimu Mkuu wa Kitengo Cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Afya Catherine Sungura imesema kuwa ni vema msafiri akauliza shirika la ndege analokwenda nalo pamoja na masharti ya nchi anayotembelea na kwa zile nchi ambazo zinahitaji kipimo cha UVIKO-19 msafiri afanye kipimo hicho ndani ya masaa 24 hadi 48 kabla ya kuanza safari.
"Hakuna sharti la chanjo ya Corona kwa wasafiri wanaokwenda nje ya nchi. Ni vema msafiri akauliza shirika la ndege analokwenda nalo pamoja na masharti ya nchi anayotembelea. Kwa zile nchi ambazo zinahitaji kipimo cha UVIKO-19 msafiri afanye kipimo hicho ndani ya masaa 24 hadi 48 kabla ya kuanza safari. Upimaji unafanyika kwa msafiri kufanya booking kupitia pimacovid.moh.go.tz ambapo atachagua kituo cha upimaji", imesema taarifa hiyo.
Taarifa imeongeza kuwa, "Baada ya upimaji majibu yatatumwa kwake kwa njia ya barua pepe aliyotumia wakati wa booking. Akifika Airport cheti hicho kitahakikiwa katika dawati la afya. Unashauriwa kujiepusha na vyeti feki".