SHIRIKA la Afya Duniani (WHO) limewatoa hofu Watanzania kuhusu chanjo ya Covid- 19 inayoendelea kutolewa nchini kote.
Mkurugenzi Mkazi wa WHO nchini Tanzania, Dk Tigest Mengestu, alisema hayo alipokutana na waandishi wa habari ofisini kwake Dar es Salaam alipotumia nafasi hiyo pia kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuonesha mfano wa kupokea chanjo hadharani hali iliyowezesha kuwapo mwitikio mzuri miongoni mwa wananchi.
Aliwatoa hofu Watanzania kuwa chanjo zinazotolewa na serikali akisema ni salama kwani moja ya jukumu la shirika hilo ni kufanya ithibati ya ufanisi na usalama wa chanjo za dharura kabla ya kuanza kutumika.
Dk Mengestu alisisitiza kuwa chanjo si mbadala wa matumizi ya vipukusi, kuvaa barakoa, kunawa mikono kwa maji tiririka au kukaa mbalimbali katika mikusanyiko.
“Kumekuwa na habari nyingi mitaani kuhusu chanjo ambazo nyingine si za kweli, ni jukumu la waandishi wa habari kupeleka taarifa sahihi kwa jamii ili iweze kuelimika na kujikinga na janga hili linaloisumbua dunia,” alisema.
Meneja wa Mpango wa Chanjo wa WHO nchini, Dk William Mwengee, alisema mtu aliyepata chanjo ana asilimia 95 ya kutopata ugonjwa huo ukilinganisha na ambaye hajapata chanjo.