Serikali imetoa Shilingi bilioni moja kwa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete kwa ajili ya kununua vifaa tiba katika hospitali hiyo.
Akizungumza Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi hiyo mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii,Prof Mohamed Janabi alisema fedha hizo zimetumika kununua mashine zinazosaidia kuboresha zaidi huduma za kibingwa chini.
Alizitaja mashine hizo kuwa ni ‘Intra-Aotic balloon Pump’ inayotumika kutibu wagonjwa wenye matatizo ya kuziba mishipa ya damu, ‘Anaesthesia Machine’ inatumika kutoa dawa ya usingizi kwa ajili ya kulaza wagonjwa wanapoingia kwenye upasuaji wa moyo, ‘ICU ECHO Machine’ ambayo inatumika kwa ajili ya kuangalia uwezo wa moyo kufanya kazi, pamoja na ‘Syringe Pumps’ ambazo hutumika kupeleka vimininika (dawa) kwenye mwili wa binadamu kupitia mishipa ya damu.
"Vifaa tiba vyote hivi vimenunuliwa kutoka fedha za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania."alisema Prof Janabi
Alisema taasisi hiyo yenye miaka mitano tangu kuanzishwa kwake imekuwa ikihudumia wagonjwa kutoka mikoa yote ya Tanzania ambao wamepewa rufaa kutoka hospitali za mikoa na za wilaya zilizoteuliwa kwa ajili ya kupata huduma ya kiwango cha juu cha tiba ya Moyo.