Dar es Salaam. Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu ameeleza kuwa Serikali ya Tanzania inatambua uwepo wa changamoto ya ndoa na mimba za utotoni na inafanya kila linalowezekana kukabiliana na hali hiyo.
Ameyasema hayo leo Ijumaa Februari 15, 2019 wakati akifungua mkutano uliowakutanisha wadau wa elimu na masuala ya jinsia ukilenga kujadili namna ya kumkwamua mtoto wa kike kwenye kizingiti cha ndoa na mimba za utotoni.
Ummy amesema takwimu zilizopo zinaonyesha watoto wa kike 27 kati ya 100 wanabeba ujauzito na kujifungia wakiwa chini ya miaka 18.
Vilevile watoto wa kike wawili kati ya watano wanaolewa wakiwa na umri wa chini ya miaka 18.
“Bado hali si nzuri na ndiyo maana Serikali inaendelea kufanya jitihada mbalimbali kuhakikisha watoto wote wanapata fursa ya kupata elimu huku tukiendelea kuwahamasisha wasirubuniwe,’
Kwa upande wake Rais wa Commonwealth of Learning (COL) Profesa Asha Kanwar amesema maendeleo hayawezi kufikiwa kama mtoto wa kike ataachwa nyuma.
Profesa Kanwar amesema kwa kutambua hilo taasisi hiyo kupitia mradi wa Inspire Girls imedhamiria kuhamasisha umuhimu wa elimu kwa mtoto wa kike na kumuweka mbali na vitu vinavyoweza kumzuia kupata haki hiyo ya msingi.
Amesema kupitia mradi huo unaotekelezwa katika nchi za Tanzania, India, Bangladesh, Msumbiji na Malawi wamefanikiwa kuwafikia wasichana 429,000 na kuwanusuru kuingia kwenye ndoa za utotoni wasichana 1,181.