Naibu Waziri wa Afya Dk. Godwin Mollel, amepongeza wadau wa Taasisi za Bima kwa kuongeza huduma za bima kwa watoto njiti katika huduma wanazotoa kwa wateja.
Dk. Mollel ametoa pongezi hizo, wakati wa hafla fupi ya makubaliano ya wadau wa Bima nchini, yaliyofanyika Dar es Salaam, ambapo sasa kampuni ya bima chini ya 'Association of Tanzania Insurers', watatoa huduma za bima kwa watoto njiti ndani ya huduma za mama na mtoto.
“Mnaweza kuona mmefanya jambo dogo sana, lakini sisi kwetu mmetusaidia sana hii, ndo maana ya kushirikiana pamoja na serikali, tunawapongeza kwa kujali maisha ya watoto njiti," amesema Dk. Mollel.
Kwa upande wao ATI, kupitia Mwenyekiti wao, Khamis Suleiman alisema: "Haikua ngumu sisi wote kukubaliana kufanikisha hili, tuliona ni jambo zuri sana na eneo ambalo lilisahaulika, kwa hiyo kwa pamoja tulikubalina tuweke gharama hizo ndani ya mfuko wa mama."