Dar es Salaam. Serikali imetoa tahadhari kuhusu mlipuko wa ugonjwa wa Ebola nchini baada ya watu 91 kuugua DRC Congo na wengine 50 kufariki dunia.
Idadi hiyo imeongezeka kutoka wagonjwa 26 katika mlipuko uliotokea Julai mwaka huu.
Akizungumza na vyombo vya habari leo Agosti 21 Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema nchi ipo hatarini kupata ugonjwa huu kwa sababu ya ujirani kati ya Congo na Tanzania lakini mpaka sasa bado haujaingia nchini Tanzania.
Ameitaja mikoa ambayo ipo hatarini kuwa ni pamoja na Mwanza, Kagera, Katavi, Rukwa na Songwe ambayo ipo mipakani.
Huo ni mlipuko wa 10 kutokea nchini DRC Congo huku wastani wa wanaoambukizwa na wanaofariki ukitajwa kuwa ni wa kiwango cha asilimia 50.