Dodoma. Serikali imenunua mashine 60 za kusafisha figo zitakazoingia nchini wakati wowote huku ikieleza tatizo lililopo sasa ni uhaba wa wataalam wa kuzitumia.
Kauli hiyo imetolewa leo Jumanne Mei 21, 2019 bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu akibainisha kuwa mashine hizo zimeagizwa Saudi Arabia ambako pia wanafanya utaratibu wa kusomesha wataalamu.
Ummy alitoa kauli hiyo wakati akijibu swali la nyongeza la mbunge wa Kilolo (CCM), Venance Mwamoto aliyetaka kujua kama Serikali ipo tayari kununua mashine za kusafisha figo na kuzisambaza katika hospitali ya Mikoa na rufaa.
Katika maelezo yake, Ummy amesema mashine hizo zitaanza kufungwa katika maeneo yasiyofikika kwa urahisi ikiwemo Mkoa wa Katavi ambako wananchi wake husafiri umbali mrefu kufuata huduma hiyo.
Mbali na mashine hizo, amesema Serikali wakati wowote itapokea magari 50 ya wagonjwa ambayo tayari yameshanunuliwa.
Katika swali la msingi mbunge wa Kinondoni (CCM), Maulid Mtulia alihoji lini Serikali itafunga mashine ya CT-SCAN na MRI katika hospitali ya rufaa ya Mwananyamala ili kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).
Pia Soma
- 24 wanusurika kifo baada ya basi walilopanda kuteketea kwa moto
- Amuua mkewe akimtuhumu kumharibu nguvu za kiume
- Jaji Ramadhan atia neno ma-DED kusimamia uchaguzi
Katika majibu yake waziri huyo amekiri umuhimu wa hospitali hiyo kutokana na kupokea wagonjwa 300,000 kwa mwaka ikilinganisha na hospitali nyingine, kusisitiza kuwa Serikali imeiweka katika hospitali zinazohitaji kuboreshwa na kuongezewa watumishi.