Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imemwita Mwakilishi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini humo, Dk Tigest Ketsela Mengestu baada ya kusambaa kwa taarifa kupitia vyombo vya habari kuhusu uwepo wa ugonjwa wa ebola Tanzania
Mwakilishi huyo amekutana na kufanya mazungumzo na Naibu Waziri wa wizara ya mambo ya nje wa Tanzania, Damas Ndumbaro leo Jumanne Septemba 24, 2019 jijini Dar es salaam
Kupitia akaunti yake ya Twitter, Msemaji Mkuu wa Serikali ya Tanzania, Dk Hassan Abbas amesema lengo la kumwita mwakilishi huyo ni kupata kwa kina hoja za shirika hilo zinazosambaa kupitia vyombo vya habari.
Katika Taarifa hiyo msemaji Mkuu wa serikali imeeleza katika mazungumzo hayo mwakilishi huyo amesisitiza WHO haijasema wala haina ushahidi wowote kuwa Tanzania kuna Ebola na itashirikiana na Serikali.
Majuma kadhaa yaliyopita nchini Tanzania zilivuma taarifa za uwepo wa ugonjwa wa ebola na taarifa zikidai kuna baadhi ya watu wameshafariki kwa ugonjwa huo lakini wizara ya afya nchini humo ilijitokeza na kukanusha taarifa hizo baada ya kujiridhisha kwa vipimo kuwa ugonjwa huo haupo Tanzania.