Serikali kupitia Wizara ya Afya inatarajia kuja na mwongozo wa gharama za kumuona daktari katika vituo vya kutolea huduma za afya vya umma nchini, ambao unatarajiwa kuanza kutumika kuanzia mwezi Februari 2023, mwongozo ambao utatoa mchanganuo wa gharama za kumuona daktari kuanzia ngazi ya zahanati, vituo vya afya, hospitali za rufaa, wilaya, mkoa, kanda, maalum na taifa.
Kauli hiyo imetolewa jana, Disemba 27, 2022 na Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu alipofanya ziara ya kushtukiza katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Temeke, kuona hali ya utoaji huduma za afya pamoja na kusikiliza kero, ushauri na maoni ya wananchi juu ya upatikanaji wa huduma za afya nchini.
Waziri Ummy amesema, hapo awali hakukuwa na mwongozo unaoainisha gharama husika za kumuona daktari, hivyo kupelekea vituo vingi vya kutoa huduma za afya kuwa na gharama tofauti tofauti zisizoendana, hivyo kuleta kero zaidi kwa wananchi.