MKUU wa Mkoa wa Geita, Rosemary Senyamule, amewaagiza viongozi na wataalamu wa afya mkoani humo kuendelea kutoa elimu ya chanjo ya Covid-19 bila kuchoka ili kuondoa dhana potofu na kuongeza mwamko wa chanjo ya Covid-19 mkoani humo.
Alisema hayo wakati akipokea taarifa ya mwendo wa utoaji chanjo katika mkoa wake.
“Niendelee kuomba na kuwasihi kwamba tuendelee kutoa elimu hiyo bila kuchoka, tuendelee kuwafafanulia kwa nini tumeletewa chanjo hii,” alisema mkuu huyo wa mkoa.
Awali mratibu wa Huduma za Chanjo mkoani hapa, Wille Luhangija alisema mkoa umepokea chanjo 50,000na wameanza rasmi utoaji wa chanjo hiyo Agosti 4.
Mganga Mkuu Mfawidhi wa Halmashauri ya wilaya ya Geita, Modest Burchard alisema ipo haja ya kuendelea kutumia gari la matangazo kutoa elimu mtaani na kupeleka huduma ya chanjo kwenye vituo vyote kama wizara ilivyoelekeza.