Amesema hayo katika taarifa aliyotoa leo Agosti 8, 2021 huku akisema kuwa, Serikali bado inaendelea kuboresha huduma za upatikaji wa vyeti kwa kukamilisha utaratibu wa kuhama kutoka kwenye mfumo wa vyeti vya makaratasi na kwenda mfumo wa kidijitali (Covid 19 Vaccine Electronic Certificates).
Amesema taarifa zote za usajili na vyeti kwa wale waliochanjwa katika vituo vya kutolea huduma za afya vya umma na binafsi vilivyoidhinishwa nchini zimeandikwa katika vitabu na baadae taarifa hizo zitahamishiwa katika mfumo wa kielektroniki.
"Serikali inatoa tahadhari iwapo kuna watu watakao jaribu kujipatia vyeti vya chanjo kwa njia za udanganyifu, kuwa watabainiwa na mfumo na kuchukuliwa hatua za kisheria,"
"Ikumbukwe kuwa, Wizara inafahamu mfuatano wa namba zake na zimetolewa kituo gani hivyo, ikitokea namba moja imejirudia uchunguzi utaanzia kwa watoa huduma waliotoa namba hizo na wateja wenye vyeti vya namba hizo" imesema taarifa hiyo.
Zoezi la kutoa chanjo ya UVIKO-19 lilizinduliwa Julai 28, 2021 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ambapo hadi kufikia Agosti 4, 2021 jumla ya dozi 1,008,400 za chanjo za UVIKO-19 zilikuwa zimesambazwa katika mikoa yote 26 na vituo zaidi ya 550 vya kutolea huduma za chanjo kwa Tanzania Bara.