Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Prof. Makubi ataka mganga mkuu asimamishwe

Makubi4 Prof. Makubi

Sun, 29 May 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Profesa Abel Makubi ameshauri kuondolewa kwa Mganga Mkuu wa Wilaya ya Kigoma kutokana na kushindwa kutekeleza maagizo ya kuboresha huduma, kukosa uwajibikaji na utovu wa nidhamu.

Aidha, mganga huyo amedaiwa kushindwa kutengeneza boti kwa gharama ya Sh1 milioni iliyokuwa ikibeba wagonjwa na wajawazito katika eneo lake.

Kwa mujibu wa kitengo cha mawasiliano Serikalini cha wizara hiyo, Profesa Makubi ametoa agizo hilo wakati akizungumza na watoa huduma za afya wa Mkoa wa Kigoma.

Amesema wapo baadhi ya waganga wakuu wa halmashauri hawawajibiki ipasavyo katika maeneo yao, wengine hawataki kutekeleza maagizo ya viongozi yenye lengo la kuboresha huduma za afya nchini na hivyo kuwarudisha nyuma.

"Miezi mitatu iliyopita Mganga Mkuu wa Serikali alitoa maelekezo ya kutengeneza boti hiyo iliyosaidia sana kubeba wagonjwa wa dharura na wajawazito.  Gharama za matengenezo ya boti hiyo ni Sh1 milioni bado mtu hutekelezi, huyu hafai kuwa kiongozi,”amesema.

Profesa Makubi amewaagiza waganga wakuu wa halmashauri kuwa wazalendo na kuwajibika ili kuongeza kasi na ufanisi katika kuboresha huduma kwa wananchi hali itakayosaidia kupunguza malalamiko yanayoweza kuzuilika.

Amesema kwa kiasi kikubwa Serikali imeboresha miundombinu katika maeneo ya kutolea huduma za afya, hivyo mkakati wa wizara kwa sasa ni kusimamia ubora wa huduma ili wananchi wanufaike na huduma hizo katika ngazi zote kuanzia zahanati mpaka hospitali maalum na Taifa.

Aidha, Profesa Makubi amewaelekeza waganga wakuu wa halmashauri kusimamia hali ya dawa katika maeneo yao ili kuondokana na changamoto ya upungufu au upotevu wowote wa dawa ili wananchi wasikose huduma hiyo.

Pia amewaelekeza waganga wakuu kuanzisha vigoda vya huduma kwa mteja kwa ambao bado hawajaanzisha, kwasababu itasaidia kusikiliza malalamiko, kero, maoni au pongezi juu ya huduma wanazotoa ili kuboresha zaidi.

Kadhalika, Profesa Makubi ameelekeza kuhakikisha wanafunga mifumo katika vituo vyao ili kuondoa changamoto ya upotevu wa mapato na dawa katika maeneo yao, hali itayosaidia katika kuboresha huduma katika maeneo yao.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live