Mwanza. Waziri Mkuu wa zamani wa Tanzania, Mizengo Pinda amesema ili kushinda vita dhidi ya maambukizi ya kifua kikuu lazima iundwe mikakati bora na kila mmoja ashiriki katika vita hiyo.
Ametoa kauli hiyo leo Novemba 29, 2019 jijini Mwanza katika tamko la viongozi wa dini kuhusu tatizo la kifua kikuu na lishe bora na kubainisha kuwa ukiondoka umaskini, maradhi na ujinga watu wataweza kuishi katika mazingira mazuri.
“Maadui wanaotusumbua bado ni umaskini, maradhi na ujinga, inashangaza sana kuona kwamba hata jiji la Dar bado kuna shida watu wengi wana maabukizi ya TB,”
“Nchi yetu bado haijafikia tunapotakiwa kufikia, wapo watu ni maskini wa kutupwa, lazima kila mmoja asimame katika jambo hili na kutengeneza mikakati ya pamoja.”
Amesema ili kufikia hatua nzuri ni vyema kuyashirikisha mashirika binafsi katika mapambano hayo ili kukaa pamoja na kuweka mikakati.
Kuhusu lishe, Pinda amependekeza watendaji wanaoajiriwa katika ngazi ya mitaa, vijiji na kata kuwa na elimu ya lishe, “kama hawana basi iwe inatolewa elimu kwao jinsi ya kushughulikia suala la lishe.”
Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema Serikali inafanya jitihada mbalimbali kuhakikisha inapunguza tatizo hilo.
Amesema awali walikuwa wakitumia darubini kuchunguza maambukizi ya kifua kikuu na majibu kupatikana baada ya saa 48 lakini kwa sasa wanatumia mashine za kisasa na majibu yanapatikana ndani ya saa mbili.