Dar es Salaam. Wananchi wameshauriwa kuwa na desturi ya kupima afya zao mara kwa mara bila kusubiri kuugua ili kuepuka gharama kubwa za matibabu na kupoteza maisha.
Ushauri huo umetolewa na Diwani wa CCM kata ya Kilungule leo Mei 19 mwaka huu Said Fella wakati wa tukio la upimaji wa afya bure liliofanyika katika kata anayoiongoza kwa udhamini wa Shirika la Uwezeshaji Kiuchumi(TDSP).
Fella amesema watu wanaangalia kutafuta chakula tu hawaangalii afya zao mara kwa mara hivyo alishauriana na Mkurugenzi wa hospitali ya Samaria Health Center na kukubaliana kuwa atakutana na madaktari wenzake ili kuwasaidia wakazi wa eneo hilo.
“Namshukuru Mungu madaktari wamejitolea kuwatibia bure wakazi wa kata yangu ambayo ina wakazi zaidi ya 66,720 na tumekusudia kuwahudumia watu 400 katika tukio hilo la siku mbili ambazo watakuwepo hapa Kilungule,” amesema Fella.
Dk, Issa Nassoro ambaye ni Mkurugenzi na Mganga Mkuu wa Hospitali ya Samaria Health Center amesema idadi kubwa ya watu wamejitokeza katika tukio hilo na mpaka sasa baadhi yao wamegundulika na ugonjwa wa kisukari, shinikizo la damu, figo na malaria.
“Upimaji ni bure kwa msaada wa madaktari na wadhamini, sisi hospitali ya Samaria tumeamua kujitolea bure bila malipo na lengo letu kufika maeneo mbalimbali hususan ambazo ziko mbali na zahanati na vituo vya afya,” amesema Dk Nassoro
Pia Soma
- Aweso achongea wakandarasi wa maji ataka wasweke mahabusu
- Kiongozi upinzani akubali kushindwa Australia
- Polisi walioharibu gari la Bobi Wine kushtakiwa
Mkurugenzi wa TDSP, Athumani Mbonde amesema shirika hilo lina kitengo cha afya hivyo wameamua kuiunga mkono Serikali kwa kuwasaidia wananchi ili waweze kupima afya zao bure.
Mbonde amesema wameanza kutoa huduma ya afya bure katika kata hiyo na baadaye wataenda wilaya ya Mkuranga na Kisarawe zilizopo mkoani Pwani.