Dar es Salaam. Anisia, pacha aliyetenganishwa na mwenzake Melnes baada ya kuzaliwa wakiwa wameungana amefariki dunia jana Jumatatu Septemba 2, 2019 katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), ikiwa ni nne tangu waliporejea nchini Tanzania kutoka Saudi Arabia walikofanyiwa upasuaji.
Akizungumza leo Jumanne Septemba 3, 2019 mkurugenzi wa huduma za upasuaji wa MNH, Dk Suphian Baruan amesema Anisia amefariki jana usiku wakati madaktari wakimpatia matibabu.
“Kama mnakumbuka tangu siku walivyorudi mmoja alionekana kuwa na tatizo, madaktari waliliona hilo na kuanza kumfanyia uchunguzi na matibabu ila nasikitika kuwataarifu kuwa amefariki,” amesema Dk Baruan.
Akizungumzia chanzo cha kifo cha mtoto huyo daktari bingwa wa upasuaji wa watoto, Petronilla Ngilino amesema wakati wanaendelea kumfanyia uchunguzi alianza kutapika.
“Ile hali ya kutapika ilitushtua lakini baada ya kumuuliza mama yake akasema alianza kutapika tangu wakiwa kwenye ndege na akawa ameishiwa nguvu.”
“Tukaanza kumuwekea maji kwa kuwa yalikuwa yanapungua, na tukazuia matapishi yasiingie kwenye mfumo wa hewa. Tuliendelea na uchunguzi tukabaini kuna tatizo kwenye tumbo lake,” amesema Dk Ngilino.
Habari zinazohusiana na hii
Amesema utumbo wa mtoto huyo ulikuwa umejifunga ndipo walipofikia uamuzi wa kumfanyia upasuaji kurekebisha hilo.“Tulifanikisha upasuaji na alipopelekwa ICU (Chumba cha Uangalizi maalum) tukaanza kuona upokeaji wake wa hewa ya oksijeni si mzuri licha ya kusaidiwa kupumua na mashine, tulijaribu kuokoa maisha yake ila usiku wa jana akatutoka,” amesema.