TAASISI ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) inatarajia kufanya utafiti kubaini kiasi cha kinga kilichozalishwa na chanjo dhidi ya Covid-19 kutoka kampuni ya Johnson & Johnson inayotumika nchini.
Mkurugenzi wa Kuratibu Mafunzo ya Utafiti wa NIMR, Dk Paul Kazyoba, alisema utafiti huo utahusisha makundi ya watu waliopata chanjo hiyo.
“Sisi kama taasisi ya utafiti ni muhimu kufuatilia masula ya utafiti, kama duniani tafiti zitafanyika na sisi pia tutafanya tafiti ili kuweza kujua zaidi chanjo hiyo na hii pia ni sehemu ya kuwajengea imani Watanzania kuwa hii chanjo inafanya kazi vizuri na hakuna haja ya kuwa na hofu. NIMR inafuatilia zaidi hatua za utoaji chanjo na vitu vingine kuhusu chanjo kwa watu,” alieleza.
Alisema taratibu za kufuatilia chanjo huwa zinaendelea kuanzia kwa wafuatiliaji wa nje hadi ndani ya nchi.
“Mfano sasa hapa tunakabiliana na wimbi la tatu kwa hiyo kama likija wimbi lingine na kutokaea mlipuko mpya, wazalishaji wa chanjo wanachunguza kama chanajo inaweza kumlinda mtu dhidi ya aina hiyo ya corona mpya,“ alisema ma kuongeza kuwa, dhidi ya Covid-19 zina faida kubwa katika kukabiliana na ugonjwa huo kwa kuwa zina protini zinazozalisha kinga mwilini.
“Bado chanjo zinamanufaa makubwa bila kujali kuna wimbi la ngapi, chanjo ya Johnson inaweza kukaa katika mazingira yetu bila kuathirika hata maeneo ya baridi kama Njombe na Kilimanjaro pia kuna utaratibu uliowekwa wa chanjo ili zihifadhiwe na tuna mifumo mizuri ya kusafirisha chanjo,” alisema.