Dar es Salaam. Mdhibiti ubora kutoka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Dk Raphael Malaba amesema watu wengi hukimbilia kujiunga na mfuko wanapoona wanahitaji huduma za afya za gharama kubwa.
Dk Malaba amesema hayo Juni 28, 2018 wakati wa mjadala wa Jukwaa la Fikra kuhusu maradhi yasiyoambukiza ulioandaliwa na Kampuni ya Mwananchi Communications Ltd (MCL).
Amesema kutokana na hali hiyo, mfuko hutoa elimu kwa wananchi ili kuhakikisha wanakuwa na bima ya afya hata kama si wagonjwa.
"Bado kuna changamoto kubwa na tunalazimika kutumia gharama kubwa kuwatibu baadhi ya wagonjwa, wakiwamo wa figo,” amesema.
Dk Malaba amesema, "Mgonjwa wa figo kwa mwaka hutumia zaidi ya Sh46 milioni kwa ajili ya kusafisha figo jambo ambalo ni gharama, ikizingatiwa kuwa wagonjwa wanaongezeka," amesema.