Dar es Salaam. Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) nchini Tanzania imeokoa Sh3.5 bilioni tangu ilipoanza kutoa huduma ya upandikizaji figo Novemba, 2017.
Akizungumza leo Agosti 2, 2019 ofisa uhusiano wa hospitali hiyo, Aminiel Aligaesha amesema tangu walipoanza huduma hiyo wagonjwa 47 wamepandikizwa figo na kugharimu Sh1.1 bilioni.
"Kama wagonjwa wote wangepelekwa nje ya nchi kwa mgonjwa mmoja ingegharimu Sh80 milioni hadi Sh100 milioni, jumla zingekuwa Sh4.7 bilioni,” amesema Aligaesha.
Amesema kwa huduma wanazozitoa kwa sasa gharama kwa mgonjwa mmoja ni Sh25 milioni hadi Sh32 milioni.
Daktari bingwa na mkuu wa idara kitengo cha figo, Jackline Shoo amesema changamoto kubwa ni kuwabaini wenye matatizo ya figo kwa maelezo kuwa wengi hufika wakiwa katika hali mbaya.
“Kwa sasa tuna wagonjwa zaidi ya 300 wanaopatiwa huduma ya kusafishwa damu na karibu nusu yao wanahitaji huduma ya kupandikizwa figo,” amesema.
Pia Soma
- Saudi Arabia yaruhusu wanawake kusafiri bila uangalizi wa mlezi wa kiume
- Mbunge Selasini asema Mbowe anapitia kipindi kigumu
- Ulega awataka wavuvi nchini Tanzania kujiunga na vyama vya ushirika