Muleba.Watoto wawili wa kike wamefariki dunia baada ya nyumba walimokuwa wamelala kuungua moto.
Ajali hiyo imetokea usiku wa kuamkia leo Agosti 7 katika katika kijiji cha Rwazi kata ya Kikuku, Kagera.
Chanzo cha moto huo kinaelezwa kuwa ni kibatari kilichokuwa kikiwaka, kuangukia godoro na chandarua.
Mwenyekiti wa kijiji cha Rwazi wilayani Muleba Wilbard Kagombora amesema wakati moto huo unashika, mama wa watoto hao alikuwa amekwenda kwa jirani kuomba chumvi.
Kagombora amesema tukio hilo limetokea jana saa 2 usiku.
“Mtoto mmoja ana umri wa miaka miwili na mwingine ana miezi sita,”amesema.
"Ndugu yao mwenye miaka minne alipiga kelele lakini mama yao alipofika alikuta nyumba imezingirwa moshi na moto mkali na kushindwa kuingia hadi ulipopungua na walipofanikiwa kuingia ndani waliwakuta watoto hao wakiwa wameteketea" ameongeza:
Amesema nyumba hiyo ilijengwa kwa tofali za udongo na kuezekwa bati lakini ndani vyumba vyote vilisambazwa nyasi za kukalia hali iliyosababisha moto kusambaa kwa kasi.
Kamanda wa polisi wa Mkoa wa Kagera Agustino Ollomi amesema amepokea taarifa hizo na akatoa rai kwa wazazi na jamii kwa ujumla kuchukua tahadhari.