Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Morogoro yapangua safu ya sekta ya afya, nane wawekwa kando

Tue, 4 Jun 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Morogoro. Timu ya watumishi nane katika sekta ya afya mkoani Morogoro imeondolewa kutokana na kushuka kwa huduma za kitabibu katika halmashauri akiwemo mganga mkuu wa mkoa huo Dk Frank Jacob.

Katibu tawala mkoa wa Morogoro, Clifford Tandari akizungumza na waandishi wa habari jana Juni 3,2019 katika ofisi ya mkuu wa mkoa wa Morogoro amesema ofisi yake kwa kushirikiana na Serikali Kuu imefikia uamuzi wa kufanya mabadiliko katika uongozi kwa sekta hiyo ya afya kwa kuondoa timu ya watumishi hao.

Tandari alisema mabadiliko hayo ni kutokana na huduma za kitabibu katika halmashauri kushuka ikiwa ni pamoja na baadhi ya hospitali na vituo vya afya madaktari kwa siku za sikukuu na mwikiendi kutofika kuangalia wagonjwa.

Alisema uamuzi huo umekuja baada ya kubainika kuwepo kwa changamoto mbalimbali ikiwemo ya rushwa na kutowasikiliza wagonjwa.

“Tutabadilisha mganga mkuu wa mkoa, Muuguzi mkuu wa mkoa, mganga mkuu wa meno na wataletwa wapya pamoja na wasimamizi wa idara mbalimbali zilizopo katika timu ya mkoa,” alisema Tandari.

Pia alisema kama mkoa umeamua kuwaleta watumishi wapya na kuwaondoa waliokuwepo nia ikiwa ni kuimarisha utendaji na watakaoletwa watapewa miongozo na kuisimamia vyema.

Pia Soma

Mkazi wa manispaa ya Morogoro Jacson Malisa ameupongeza uongozi wa mkoa wa Morogoro kwa kufanya mabadiliko katika sekta ya afya kwani yataleta tija na kuleta ufanisi katika sekta hiyo kwani kumekuwa na malalamiko ya muda mrefu.

“Mamlaka zilizofanya hivyo zisisite pindi zitakapoona kwamba kuna masuala ambayo yanajirudia kati ya hawa walioondolewa na hii italeta uwajibikaji, hata waliondolewa wakafanye kazi kwa maelekezo yanayotakiwa,” alisema.

Chanzo: mwananchi.co.tz