TAASISI ya Mifupa ya Hospitali ya Taifa Muhimbili (MOI) imesema katika kipindi cha miaka minne chini ya uongozi wa Rais John Pombe Magufuli wamefanya upasuaji wa kibingwa kwa wagonjwa 43,200 kwa gharama ya Shilingi bilioni 16.5.
Hayo yamesemwa na daktari bingwa wa mifupa, Vivina Wananji wakati akiwasilisha ripoti kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii chini ya Mwenyekiti wake, Stanslaus Nyongo.
Dk Vivina alisema iwapo wagonjwa hao wangepelekwa nje ya nchi matibabu yao yangeigharimu serikali zaidi ya Shilingi bilioni 54 hivyo kuokoa bilioni 38.4
Amesema serikali ya awamu ya tano imetoa kiasi cha Shilingi bilioni 7.9 kwa ajili ya ujenzi wa maabara ya kisasa ya upasuaji wa ubongo (Ango-Suite).
“Maabara hii itaiwezesha taasisi kufanya upasuaji wa matatizo ya mishipa ya damu kichwani pasipo kulazimika kufungua fuvu la kichwa, vilevile mashine hii itakua na uwezo wa kutibu damu iliyoganda kwenye mishipa ya damu miguuni, kwenye moyo, tumbo la uzazi, ini na figo” amesema Dk Vivian
Dk Vivina amefafanua kuwa matibabu kwa kutumia maabara hiyo ni ya haraka hivyo wagonjwa wengi watapata huduma kwa muda mfupi huku uwepo wa maabara hiyo utaifanya Tanzania kuwa moja ya nchi chache barani Afrika zinazotoa huduma hiyo.