Ukiwa mjamzito au unanyonyesha mwili wako unahitaji mlo unaotokana na vyakula vya aina mbalimbali.
Hata hivyo vyakula kila siku husaidia mwili kupata nguvu na virutubisho vyote unavyohitaji wewe na mtoto wako. Medina Wandella ni ofisa mtafiti mwandamizi wa elimu na mafunzo ya lishe kutoka Taasisi ya Chakula na Lishe(TFNC) anasema lishe bora huzuia upungufu wa damu.
“Lishe bora hupunguza uwezekano wa kupata mtoto mwenye uzito pungufu, kujifungua kabla ya wakati au kupata mtoto mfu,” anasema.
Pia, anataja vyakula vinavyotakiwa katika mko kamili kuwa ni vya nafaka, viazi, mihogo na ndizi.
Vyakula vingine ni vya jamii ya kunde, vyenye asili ya wanyama, matunda, mbogamboga, mafuta na sukari. “Mafuta yakiongezwa kwenye mbogamboga na vyakula vingine huboresha ufyonzaji wa baadhi ya vitamini na huongeza nguvu mwilini,” anasema Wandella.
Anafafanua kuwa mboga za majani zinatakiwa zioshwe vizuri na maji safi kabla ya kukatwatwa, lakini zipikwe mara moja kwa muda mfupi na kuliwa mara baada ya kupikwa ili kuhifadhi virutubishi vilivyopo katika mboga hizo. “Kwa upande wa matunda na mbogamboga zinazoliwa bila kupikwa zinatakiwa zionywe vizuri kabla ya kuliwa ili kuepuka magonjwa ya kuhara ,” anasema.
Pia Soma
- SADC MKUTANO MKUU 2019: Kawawa aeleza jinsi walivyoishi na wapigania uhuru
- Watu zaidi ya 57 wafariki dunia baada ya lori la mafuta kulipuka Morogoro
- Kortini kwa kusafirisha mirungi kilo 500.
Mtaalamu huyo anasema wajawazito na wanawake wanaonyonyesha hawatakiwi kutumia pombe, dawa za kulevya, bidhaa zenye tumbaku au vinywaji vyenye kafei kwa sababu ni hatari kwa afya.
Mtaalamu huyo anashauri unywaji wa maji wa na utumiaji wa chumvi yenye madini joto kwa afya.
Makala haya yameandikwa na mwandishi wa gazeti hili, Hadija Jumanne