Dar es Salaam. Mwenyekiti wa chama cha madaktari wanawake (Mewata), Dk Faraja Chiwanga amesema upo uwezekano wa mtoto kupata maradhi yasiyoambukiza kama vile kisukari endapo mjamzito hatazingatia kanuni za afya.
Dk Faraja amesema hayo wakati wa mjadala wa Jukwaa la Fikra ulioangazia maradhi yasiyoambukiza ulioandaliwa na Kampuni ya Mwananchi Communications Ltd (MCL) wachapishaji wa magazeti ya Mwananchi, The Citizen na Mwanaspoti.
Amesema afya ya mtoto inatakiwa kulindwa tangu akiwa tumboni ili kumuepusha na madhara anayoweza kuyapata.
"Zingatia afya, fuata kile kinachotakiwa ili kuhakikisha unamkinga mtoto, katika hili afya ya mama na mtoto ni ya kuzingatiwa," amesema Dk Faraja.