Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mjadala Chanjo: Kauli ya WHO, Hatua zake kwa kina na jinsi zinavyotengenezwa

FFWREYT6R Mjadala Chanjo: Kauli ya WHO, Hatua zake kwa kina na jinsi zinavyotengenezwa

Thu, 18 Nov 2021 Chanzo: Nipashe

WAKATI dunia inahaha kuhakikisha chanjo iliyokwishapatikana dhidi ya maradhi ya corona inasambazwa duniani, Shirika la Afya Duniani (WHO), lina ufafanuzi wa undani wake unavyotengenezwa.

Kimsingi, chanjo inaundwa na vipande vidogo na chembe za ujumbe zinazosababisha magonjwa, sambamba na viungo vingine vinavyosaidia chanjo kuleta ufanisi.

Viungo vingi kila kimoja kinatumika kwa kusudi maalum. Hapo, kila kimoja hujaribiwa katika mchakato wa utengenezaji na inafanyiwa majaribio kwa sababu za usalama. Vifahamu viungo hivyo:

Antigeni: Kimsingi inasaidia kinga mwilini dhidi ya magonjwa. Inaundwa na sehemu ndogo ya viumbe vinavyosababisha magonjwa (bakteria, virusi, ‘pollen’) dhidi ya hitaji kama protini au sukari.

Vihifadhi: Inazuia chanjo kuharibika au kuchafuliwa baada ya kufunguliwa kizibo. Pale itatumika kuchanja mtu zaidi ya mmoja.

Zingine hazina hifadhi kwa sababu zinawekwa kwenye kasha ya dozi au kipimo kwa ajili ya mtu mmoja na inatupwa baada ya chanjo kutumika.

Vidhibiti: Kemikali kutoka machoni inayoweza kuwa sukari, tindikali amino na protini mwilini mwa binadamu, inayotokana na hamira au chachu.

Surfactants: Chembe inayoweka viungo vyote kwenye chanjo na inasaidia kutulia, au vitu vilivyoko kwenye mfumo wa maji kutogongana. Pia, hutumika katika vyakula kama barafu.

Mabaki; ni kiasi kidogo cha vitu vinavyotumika kutengeneza au huzalisha chanjo ambazo sio viungo hai katika chanjo iliyokamilishwa.

Vitu vinatofautiana kulingana na mchakato wa utengenezaji uliotumika na vinaweza kujumuisha protini za mayai, hamira au viuatilifu na athari za mabaki hayo, inatajwa kuwa ndogo sana mwilini.

Diluent-kimiminika; ni maji yanayotumika kulainisha chanjo katika usahihi unaohitajika kabla ya matumizi. Kimiminika kinachotumiwa zaidi ni majisafi.

Adjuvant-visaidizi; aina ya visaidizi vinavyoimarisha kinga kuhimili chanjo na kuifanya sindano ya chanjo ikae mwilini muda mrefu au kuamsha chembe za kinga.

Visaidizi hivyo, pia vinaweza kuwa vya kiwango kidogo cha chumvi chenye mjumuiko wa kemikali kama vile ‘aluminium phosphate.’

CHANJO INAVYOTENGENEZWA

Kila chanjo ni lazima ipitie majaribio ya kina, kuhakikisha usalama kabla haijaanza kutumika rasmi.

Inafanyiwa uchunguzi kubaini namna itakavyotumika kuamsha kinga, kisha inajaribio kwa wanyama, kutathmini usalama wake na uwezo wa kuzuia magonjwa na inapoleta mwitikio, ndio inafuata awamu ya kujaribiwa kwa binadamu katika awamu kuu tatu:

Mosi; chanjo hutolewa kwa idadi ndogo ya watu waliojitolea kuthibitisha ubora wake na kupata kipimo sahihi, ikihusisha vijana na watu wazima wenye afya njema.

Pili; Chanjo inatolewa kwa umma uliojitolea kutathmini zaidi usalama na uwezo wake kujenga kinga. Washiriki hapo wanakuwa na sifa sawa kama vile umri, jinsia, kulingana na walivyokusudiwa. Majaribio hayo ni ya kutathmini makundi ya umri na vigezo vinginevyo.

Kundi ambalo halikupata chanjo, kwa kawaida hujumuishwa katika awamu hiyo ikiwa na kikundi linganishi ambacho hakijachanjwa, kubaini mabadiliko.

Tatu: Kuna kundi kubwa zaidi hata idadi ya maelfu waliojitolea, wakilinganishwa na kundi kama hilo la wasiopata chanjo. Muhimu ni kubaini usalama wa chanjo tajwa.

Majaribio mengine ya awamu ya tatu hufanywa katika nchi tofauti na sehemu nyingi za nchi husika, ili kupata uhakika wa utendaji wa chanjo hiyo kwa umma.

Kimsingi, majaribio ya awamu ya pili na tatu ya waliojitolea na wanasayansi wanaoendesha utafiti, hufichwa kujua na kupata uhalisia wa kina, ikipewa msamiati “kupofusha.”

UNDANI UNAVYOSHUGHULIKIWA

Baada ya majaribio na matokeo yote kukamilika, waliojitolea na wanasayansi walioendesha majaribio wanaarifiwa ni nani aliyepata chanjo hiyo.

Maofisa katika kila nchi hutathmini kwa kina takwimu za majaribio na kuamua ama waidhinishe chanjo hiyo kwa matumizi au la.

Chanjo lazima ithibitishwe kuwa salama na yenye ufanisi kwa watu wengi, kabla ya kuidhinishwa na kuingizwa kwenye programu za kitaifa za chanjo.

Baada ya hapo, ufuatiliaji zaidi unafanyika kukitumika mifumo sahihi ya usalama na ufanisi wa chanjo zote, hata kuwezesha wanasayansi nao kuwa na ufuatiliaji wao, wakitathmini kiwango kinachotumiwa na jamii ngazi ya juu au kidogo.

Takwimu hizo hutumiwa kurekebisha sera za matumizi ya chanjo, ili kuongeza athari zilizopo, pia kuruhusu chanjo kufuatiliwa kwa usalama kupitia wakati wote wa matumizi yake.

Wakati chanjo inapoanza kutumika, ni lazima ifuatiliwe kila wakati kuhakikisha inadumu kuwa salama.

VITA CORONA

Mnamo Machi mwaka huu, WHO ilitangaza hakuna sababu ya kusitisha matumizi ya chanjo ya AstraZeneca, kwa kuhofia madai yanayotolewa kama vile kuganda damu ya mhusika, kwa kukosa ukweli unaohusiana madai hayo yanayosambaa.

Ni taarifa kwa mataifa kama Bulgaria, Denmark na Norway zilisitisha matumizi ya chanjo hiyo, kama ilivyo kwa Thailand, Italia na Austria zilizositisha kwa tahadhari.

WHO inahimiza hakuna uhusiano kati ya chanjo hiyo na hatari ya damu kuganda na mtaalamu wake, Dk. Margaret Harris, anaitetea chanjo ni salama na iendelee kutumika, akifafanua imeshawafikia watu milioni tano barani Ulaya, hadi miezi nane iliyopita.

Kulikuwapo madai ya watu 30 barani Ulaya kupata madhara ya kuganda damu, ikiainishwa na kifo cha mama mwenye miaka 50, baada ya chanjo.

WHO inatamka kuendelea na uchunguzi dhidi ya madai hayo, ingawa Dk. Harris anasisitiza hakuna uhusiano wowote na matatizo ya kiafya yaliyoripotiwa.

Mataifa ya Bulgaria, Denmark, Iceland ziliacha kuendelea na dozi ya kinga, pia Norway, Thailand, Italia na Austria zilichukua hatua kama hiyo kwa tahadhari.

"Niliagiza kusitishwa kutolewa kwa chanjo ya AstraZeneca mpaka Wakala wa dawa Ulaya atakapotuthibitishia hakuna shaka yoyote iliyopo juu ya usalama wa dozi hiyo," anasema Waziri Mkuu wa Bulgarian, Boyko Borisov.

Shirika la Dawa la Muungano wa Ulaya (EMA), lilisema awali hakukuwapo dalili za chanjo hiyo kusababisha kuganda damu mwilini, ikihimza faida zake ni kubwa kuliko hatari zake.”

Pia kunaelezwa kufanyika utafiti mkubwa katika majaribio ya tiba katika maabara za Ureno, Australia, Mexico na Ufilipino, wanakoendelea na mpango wa utoaji chanjo.

Mataifa mengine ambayo yanaendelea kutoa chanjo hiyo ni Uingereza, Ujerumani, Mexico na Australia.

HAKUNA USHAHIDI

Nchini Uingereza, Shirika la Udhibiti wa Bidhaa za Huduma za Afya (MHRA), limesema hakuna ushahidi wa kuwapo chanjo iliyosababisha matatizo na watu wananapaswa kuendelea kuchanjwa wanapoombwa kufanya hivyo.

Zaidi ya dozi milioni 11 za chanjo ya AstraZeneca zimekwishatolewa Uingereza kwa mujibu wa MHRA, huku Ureno inasema faida za chanjo zinaendelea kuwa kubwa kuliko athari zake kwa wagonjwa.

HALI INAVYOFANYA KAZI

Chanjo ya AstraZeneca iliyotengenezwa na Chuo Kikuu Oxford, Uingereza kutokana na virusi vinavyosababisha mafua ya kawaida iliyodhoofishwa, inafahamika kwa jina ‘adenovirus’ kutokana na sokwe.

Ni virusi vilivyobadilishwa umbo vikaonekana zaidi mithili ya corona, ingawa haviwezi kusababisha ugonjwa. Mtu anapochomwa chanjo hiyo, inaunda mfumo wa kinga mwilini, jinsi ya kupambana na virusi halisi, pale utakapohitaji kufanya hivyo.

Chanzo: Nipashe