Mkoa wa Katavi umeripotiwa kuwa na mtu mmoja aliyegundulika kuwa na ugonjwa wa kipindupindu. Mtu huyo amebainika katika Halmashauri ya Mpimbwe wilayani Mlele.
Kutokana na hali hiyo, wananchi wameiomba Serikali kusisitiza suala la usafi kwenye makazi na maeneo ya biashara ikiwemo kuzoa taka kwa wakati.
Wakizungumza na Mwananchi leo Jumamosi Januari 27, 2024 baadhi ya wananchi wa Manispaa ya Mpanda, wamesema Serikali isipochukua hatua, ugonjwa huo utaiathiri jamii kwa kiasi kikubwa.
Ofisa afya wa Manispaa ya Mpanda, Erick Kisaka amesema wanaendelea kuielimisha jamii kufanya usafi na kunawa mikono mara kwa mara.
"Tunapita kaya kwa kaya kukagua na uchafu uliopo kwenye masoko umeanza kuzolewa, magari yameongezeka badala ya kutumia moja,"amesema Kisaka.
Mkuu wa mkoa huo, Mwanamvua Mrindoko ametoa onyo kali kwa wakuu wa wilaya, wakurugenzi watendaji na maofisa afya kuhakikisha wanasimamia usafi.