Dodoma. Matukio ya ubakaji yameongezeka Tanzania katika kipindi cha Desemba 2015 kutoka 394 hadi kufikia 2,984 kwa Desemba 2017 ambalo ni ongezeko la matukio 2,590.
Akijibu swali leo Jumatano Mei 15, 2019 Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Faustin Ndugulile amesema Serikali inaendelea kufanya jitihada mbalimbali za kuzuia vitendo hivyo.
Dk Ndugulile alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum (CCM) Najma Giga ambaye ametaka kujua tokea kupitishwa kwa sheria ya makosa ya kujamiiana (Sospa) ya mwaka 1998 ubakaji umepungua au kuongezeka.
Mbunge huyo amehoji Serikali ina mpango gani mpya katika kupambana na kutokomeza ubakaji Tanzania.
Naibu Waziri amesema Serikali imechukua hatua mbalimbali katika kukabiliana na ukatili dhidi ya watoto ikiwemo kuanzishwa kwa kamati za 10,988 ulinzi wa wanawake na watoto, na vikundi vya malezi 1,184.
Dk Ndugulile amesema Serikali iliweka sheria hiyo ambayo inatoa adhabu ya kifungo cha miaka 30 jela au kifungo cha maisha.
Pia Soma
- Kisena wa Udart, wenzake wafutiwa mashtaka
- Serikali yatenga mabilioni kulipa fidia maeneo ya jeshi
- Mgomo wa madereva wa mabasi watua bungeni, Dk Tulia atoa agizo kwa Serikali
Naibu Waziri amesema tayari Serikali imeandaa mpango kazi wa taifa wa kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto 2017/18- 2021/22 ambayo kupitia mpango huo inatoa pia elimu bure.
Kwa mujibu wa Naibu Waziri, wanaofanya matukio hayo wengi huwa wanatoka karibu na familia au ni ndugu wa watoto.