SERIKALI imeweka mpango Mkakati wa kupunguza kiwango cha malaria kutoka asilimia 7.5 mwaka 2017 hadi kufikia asilimia 3.5 ifikapo mwaka 2030
Mpango huo ni kuhimiza matumizi ya vyandarua vyenye dawa, upuliziaji viuatilifu, uangamizaji wa viluilui, viuadudu na kudhibiti mazingira.
Pia upimaji na kutoa matibabu sahihi pamaoja na kusambaza tiba kinga.
Naibu Waziri wa wizara hiyo, Dk Godwin Mollel amesema hayo wakati akijibu swali la Maida Hammad Abdallah, Mbunge wa Viti Maalum (CCM) Mkoa wa Kaskazini Pemba aliyetaka kujua jitihada zinazofanywa na serikali katika kupunguza malaria.
Mollel alisema mkakati huo ni kutokomeza kabisa ugonjwa wa Malaria ifikapo 2030 ambapo kwa kushirikiana na wadau serikali imekuwa ikitekeleza mikakati mbalimbali ya kudhibiti ugonjwa huo nchini.
Alisema kufanikiwa kupunguza kiwango cha maambukizi ya Malaria kutoka asilimia 40 mwanzoni mwa miaka 2000 mpaka asilimia 7.5 mwaka 2017 ni moja ya ishara nzuri ya kufanikisha mambapambo hayo.
Kwa mujibu wa Takwimu za Wizara ya Afya, ya mwaka 2017/2018, zinaonesha kiwango cha maambukizi ya ugonjwa huo kupunguwa kwa asilimia 7.3 ikilinganishwa na matokeo ya tafiti ya mwaka 2015.
Ugonjwa wa malaria ni kati ya maradhi yanayosababisha vifo vingi nchini ambapo kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2017/2018, katika kila wagonjwa 1,000 wa malaria, tisa kati yao hufariki dunia na makundi ya jamii yaliyo katika athari kubwa ya malaria ni watoto na wajawazito.