Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amegawa kadi za bima ya afya ya Mfuko wa Jamii (CHF) kwa watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu 625.
Amesema bima hizo ni zawadi ya sikukuu za Krismasi, mwaka mpya na Maulid baada ya kubaini changamoto ya matibabu kwa watoto.
Akigawa kadi hizo leo Jumamosi Desemba 14, 2019, Makonda amesema uandaaji wa bima hizo kwa watoto umewezekana kutokana na ufadhili wa nchi za Falme za Kiarabu.
"Niliwaza sana kwamba niandae chakula ili nile na watoto yatima? Nikaona tutakula siku moja itaisha lakini kadi hizi watatibiwa kwa mwaka mzima popote watakapokuwa nchini,” amesema Makonda.
Amesema balozi wa Falme za Kiarabu, Khalifa Abdulahman Almarsouqi alipomtembelea na kuuliza eneo la kusaidia, aliwakumbuka watoto hao akaomba kuungwa mkono kuhusu bima za afya.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Dk Yudas Ndungile amesema bima walizopewa zitawasaidia watoto kutibiwa kwenye zahanati, vituo vya afya, hospitali za wilaya na mikoa.
"Hata hivyo bado watoto wengi wana uhitaji," amesema Dk Ndungile.