Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Majaliwa aipa ushauri Hospitali ya Aga Khan

45831 Pic+aghakan Majaliwa aipa ushauri Hospitali ya Aga Khan

Mon, 11 Mar 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Serikali imeutaka Mtandao wa Maendeleo wa Aga Khan (AKDN), ufanye mapitio ya gharama za afya katika Hospitali ya Aga Khan ili wananchi wa kawaida waweze kumudu na kunufaika na huduma za tiba wanazozitoa.

Imeelezwa pamoja na jitihada za Serikali za kuboresha huduma za afya, pia inatambua mchango unaotolewa na taasisi zisizo za Kiserikali ikiwemo Hospitali ya Aga Khan katika kuimarisha upatikanaji wa huduma za kisasa.

Hayo yamesemwa leo Jumamosi, Machi 9, 2019 na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati wa ufunguzi wa awamu ya pili ya upanuzi wa Hospitali ya Aga Khan jijini Dar es Salaam kwa niaba ya Rais wa Tanzania, John Magufuli.

Amesema upanuzi wa hospitali hiyo ni miongoni mwa jitihada za kuwafikishia Watanzania huduma za afya katika maeneo yao na kwa ngazi zote na kwa gharama nafuu, hivyo amewataka watoa huduma wote nchini waangalie upya gharama zinazotozwa katika huduma mbalimbali hususan za matibabu. 

 

“Mtakubaliana nami kuwa gharama zikiwa kubwa hazitawanufaisha wananchi hususan wa kipato cha chini na wananchi hawataona unafuu wa kutibiwa nchini na nje ya nchi, hivyo fanyeni mapitio ya gharama hizo,” amesema.

 

Waziri Mkuu amesema Serikali inatambua gharama kubwa za uwekezaji na uendeshaji wa shughuli za afya nchini hususan kwa sekta binafsi.

 

“Lengo la Serikali kutoa misamaha ya kodi kwa baadhi ya taasisi zisizo za kiserikali kama Aga Khan ni kuwezesha huduma zinazotolewa kuwa nafuu,” amesema.

 

Wakati huo huo, Waziri Mkuu amesema Serikali imeanzisha na kuhamasisha wananchi kujiunga na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) na mwitikio ni mkubwa huku lengo likiwa kuhakikisha kila mwananchi anapata fursa ya matibabu tena kwa uhakika. 

 

“Nitoe wito kwa taasisi zote zisizo za Serikali kuunga mkono jitihada hizi za Serikali na kuhakikisha wananchi wote wananufaika na huduma zenu kupitia mfumo huu bila kubaguliwa,” amesema.

 

Pia ameutaka uongozi wa Hospitali ya Aga Khan na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya wakamilishe majadiliano yao katika matumizi ya NHIF kwenye hospitali hiyo ya rufaa, “Dk Konga Mkurugenzi Mkuu wa NHIF upo hapa kamilisheni mjadala.” 

Amesema nia ya Serikali ni kuona wananchi wanakwenda hapo kwenye jengo hilo zuri na wanapata huduma kupitia bima ya afya.

 

“Ni matumaini yangu kwamba jambo hili litafanyiwa kazi kwa kuzingatia maslahi mapana ya pande zote mbili,” amesema.

 

Waziri Mkuu pia amesema Serikali itaendelea kuhakikisha uwepo wa mazingira mazuri ya uwekezaji, kuimarisha amani na utulivu, ambapo ametoa rai kwa sekta binafsi ziendelee kuunga mkono jitihada za Serikali katika kutekeleza shughuli mbalimbali za maendeleo nchini kwa kuzingatia sheria za nchi, utamaduni na mila za Watanzania. 

 

Awali, Waziri Mkuu alitembelea maeneo mbalimbali ya kutolea huduma katika jengo hilo ikiwemo maabara, chumba cha upasuaji, wodi ya watoto na wodi ya wazazi.

 

Ujenzi wa hospitali hiyo umegharimu Sh192 bilioni, kati yake Sh134 bilioni ni mkopo wa muda mrefu wenye masharti nafuu kutoka Shirika la Maendeleo la Ufaransa (AFD).

 

Kwa upande wake, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu ameupongeza Mtandao wa Maendeleo wa Aga Khan kwa upanuzi wa hospitali ya Aga Khan jijini Dar es Salaam kwani unakwenda kuboresha huduma za afya nchini.

 

Amesema Serikali inatambua mchango mkubwa wa mtandao huo katika maeneo mbalimbali yakiwemo ya kutolea huduma za afya ambapo kwa sasa imeanzisha ushirikiano na sekta ya umma na binafsi kwenye mikoa ya Dar es Salaam na Mwanza. 

 

Naye, Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania, Balozi Frederic Claiver amesema awamu ya pili ya upanuzi wa hospitali hiyo itasaidia kuboresha utoaji wa huduma za afya Tanzania.

 

Pia Balozi huyo amesema Ufaransa itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kuhakikisha inatimiza mkakati wake wa kukuza uchumi kutoka wa chini kwenda wa kati kupitia sekta ya viwanda ifikapo 2025.

 

 



Chanzo: mwananchi.co.tz