Dar es Salaam. Chama cha Madaktari Tanzania (MAT) kimeiomba Serikali kuwahakikishia madaktari na wauguzi vifaa vya kujikinga na ugonjwa wa virusi vya corona, Covid-19 ili wasipate maambukizi.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Alhamisi Aprili 2, 2020, Rais wa chama hicho, Dk Elisha Osati amesema vifaa vya kujikinga ni muhimu kwao ikizingatiwa idadi ya wagonjwa na walio katika hatari ya kupata maambukizi inaongezeka siku hadi siku.
"Tunadhani kuna nguvu inatakiwa kuongezwa hivyo tahadhari ni muhimu sana kwa sababu dunia nzima wanalia na uhaba wa vifaa," amesema Dk Osati.
Ameishauri Serikali kupunguza msongamano wa wagonjwa kwenye kliniki za magonjwa mengine kama kisukari na ukimwi kwa kutoa dawa za muda mrefu.
"Mfano wagonjwa wale wa kisukari, shinikizo la damu, maumivu migongo na misuli wanaweza kupewa dawa walau za miezi mitatu kwa Sababu hawa wana uwezekano wa kupata ugonjwa mkali zaidi," amesema.
Dk Osati ameipongeza Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara ya Afya , kwa namna wanavyoongoza nchi kupambana na ugonjwa huo.