Tabora. Kanisa Katoliki Jimbo kuu la Tabora limeanzisha utaratibu wa kuwaita madaktari katika misa ili kuwapa elimu waumini jinsi ya kujikinga na ugonjwa wa virusi vya corona, Covid-19.
Akizungumza katika maombi maalum ya viongozi wa dini mkoani Tabora, Askofu mkuu wa jimbo hilo, Paul Ruzoka amesema wanataka kuwalinda waumini wao na Watanzania.
Amesema utaratibu huo utawapa uelewa mkubwa waumini wa kanisa hilo na wataweza kujikinga na ugonjwa huo.
Askofu Ruzoka amesema hatua walizochukua ni kuweka maji na vitakasa mikono nje ya makanisa sanjali na kuwahimiza waumini wao kuweka vitu hivyo na kufuata maelekezo ya wataalamu wa afya.
Amemuomba mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri kuwa kanisa hilo litatii maelekezo yote ya Serikali kuhusu ugonjwa huo kwa lengo la kuwakinga waumini na wananchi.
Amesisitiza kwamba kanisa katoliki lina sala maalum ya kuomba huruma ya Mungu ambayo waumini wanaisali katika ibada nchi nzima lengo likiwa ni kumuomba Mungu aliepushe Taifa na dunia dhidi ya ugonjwa huo.
Pia Soma
- Madaktari, wauguzi Tanzania waomba vifaa kujikinga na corona
- Wagombea CCM walivyopita chujio uchaguzi wa 1980
- Mbio za urais Zanzibar zahamia mitandaoni
Awali, mganga mkuu wa Mkoa wa Tabora, Dk Honoratha Rutatinisibwa aliwaeleza viongozi wa dini mkoani Tabora kuwa hadi sasa wameambukizwa watu ishirini na mmoja amefariki.