Dar es Salaam. Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Tiba ya Mifupa Moi, Dk Respicious Boniface leo amefungua kongamano la kimataifa la madaktari wa mifupa linalofanyika kwa siku tano hapa nchini ambapo madaktari zaidi ya 150 kutoka mataifa ya Afrika na sehemu mbalimbali duniani wanashiriki.
Madaktari bingwa wa mifupa kutoka nchi za Kusini, Mashariki na Magharibi mwa Afrika ikiwemo Ghana, Nigeria na kwingineko wanashiriki kongamano hilo.
Kongamano hilo limeratibiwa na Taasisi ya Moi kwa kushirikiana na taasisi za IGOT, SIGN, OTA na Chuo Kikuu cha California San Fransisco, Marekani.
Dk Boniface amesema kongamano hilo limekua likifanyika hapa nchini kila mwaka kwa lengo la kuwajengea uwezo na kuwapa mbinu mpya za matibabu ya mifupa madaktari hapa nchini na nchi nyingine barani Afrika kutokana na Moi kuwa kituo cha mafunzo baada ya kuwa na huduma bora za mifupa inazozitoa.
“Madaktari bingwa nchini wamekua wakinufaika na kongamano hili, wamekua wakipewa mbinu mpya na za kisasa za matibabu na upasuaji wa mifupa jambo ambalo limesababisha Moi kuweza kumaliza rufaa za nje ya nchi kwa wagonjwa wa mifupa ambapo kwa sasa huduma karibu zote zinapatikana hapa nchini,” amesema Dk Boniface.
Mratibu wa kongamano hilo Dk Joseph Mwanga amesema mafunzo yatatolewa kwa njia ya nadharia na vitendo katika chumba cha maabara kwa kutumia mifupa bandia na kwenda kwenye chumba maalum cha kujifunzia cha maiti.
Pia Soma
- MADAI: DPP awatuhumu wabunge kwa rushwa, Spika ajibu
- Wafanyabiashara walia bei ya mifuko mbadala
- Hukumu kesi ya Lucky Vincent kusomwa kesho
- Wabunge washangazwa kutolea Sh100milioni za maendeleo badala ya Sh19.6bilioni bajeti Wizara ya Madini