KIONGOZI wa upinzani, Raila Odinga, amewatahadharisha Wakenya juu ya siasa za kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2022, akiwataka wawe makini na aina ya watu wanaotaka kuwania urais.
Aidha, kiongozi huyo amewataka Wakenya kujiandaa na mabadiliko makubwa ya kisiasa kuelekea uchaguzi huo. Ameonya kuwa watakaoguswa katika mabadiliko hayo, watulie na wasijaribu kuyazuia kwa sababu yatawagharimu.
Odinga ambaye ni Kiongozi wa chama cha Orange Democratic Movement (ODM) aliyasema hayo katika sherehe za kumkaribisha nyumbani, zilizoandaliwa na Mbunge wa Nyatike, Tom Odege.
“Huwezi kuyakataa mabadiliko, wala huwezi kuyazuia mabadiliko chanya katika jamii. Ukijaribu tu, yatakuondoa,” alisema katika mkutano wa hadhara kwenye viwanja vya Nyatike.
Kuhusu kampeni ya kupambana na rushwa na walanguzi inayoongozwa na Rais Uhuru Kenyatta, Odinga alisema hahofii kampeni hiyo na kwamba anaiunga mkono.
“Kazi anayofanya Rais Kenyatta ninaiunga mkono na inastahili iwe endelevu kwa maslahi ya wananchi wa Kenya. Mimi na Rais Kenyatta tunajaribu kuyatibu maumivu ambayo nchi hii ilipitia kutokana na mambo ya kisiasa,” alisema Odinga.