Dar es Salaam. Bohari Kuu ya Dawa (MSD) nchini Tanzania imesambaza lita 350,000 za visafisha mikono pamoja na vifaa vingine ikiwamo vifunika pua (mask) kwa mashirika na taasisi mbalimbali ambazo zimeomba.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatano Machi 18,2020, Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Laurean Bwanakunu amesema idadi hiyo inatokana na uhitaji wa Watanzania kujikinga na maambukizi ya virusi vya corona (CODIV-19) uliongia nchini humo.
“Tumesambaza vifaa hivyo katika vituo vya afya ambako ndiko kwenye hatari zaidi, lakini pia kwenye maduka makubwa ili watu waweze kununua,” amesema Bwanakunu
Amesema kutokana na uhitaji wamepokea oda nyingi kutoka taasisi za umma na binafsi zikihitaji vifaa hivyo.
“Kuna taasisi kama 45 zimeleta mahitaji yao na tunashughulika nayo ila kwa Mtanzania mmoja mmoja watakwenda kununua kwenye maduka makubwa,” amesema
Bosi huyo wa MSD ametaja baadhi ya maduka makubwa kuya ni yale yaliyopo Muhimbili (Dar es Salaam, Katavi, Chato (Geita) na Ruangwa (Lindi).
Habari zinazohusiana na hii
- Watafiti Uganda wagundua virusi vya corona kwenye mwili wa ngamia na popo
- VIDEO: Serikali ya Tanzania yavifunga vyuo vyote kwa siku 30
- Wanafunzi baadhi ya Shule Arusha waenda shule
- UDSM yatoa saa 48 wanafunzi wote kuondoka
Kuhusu kupanda bei za vifaa hivyo katika maduka mbalimbali nchini, bosi huyo alisema kinachofanyika kwa sasa ni biashara baada ya watu kuona ugonjwa huo umeingia.
“Hivi vifaa vilikuwapo tangu zamani ila watu kupitia ugonjwa huu wameamza kufanya biashara bei zetu halali ni Sh85,000 kwa ujazo wa lita tano za vitakasa mikono, Sh 18,000 kwa lita moja, Sh5500 kwa mililita 250, Sh3000 kwa mililita 100 na Sh1500 kwa mililita 100. Lakini hivi sasa unakuta mtaani huko wanauza lita tano kwa Sh150,000,” amesema
Kuhusu watu kuuziwa visafisha mikono bandia, amesema si uungwana kufanya hivyo na Serikali itaona namna gani ya kulishughulikia suala hilo.
“Vifaa vyetu vinakaguliwa na (Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba) TMDA kuangalia kuwa siyo bandia hivyo tunaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu vifaa vyetu lakini pia niwaambie wananchi kuwa wasipende kununua vifaa mitaani vinaweza kuleta madhara hivyo ni vyema wanunue katika maduka makubwa yanayotambulika,” amesema
“Wananchi waendelee kufuata maelekezo yanayotolewa na wizara ya afya si lazima kutumia viziba pua ama kutumia visafisha mikono, vifaa hivi vinatumika,” amesema
Endelea kufuatilia Mwananchi kwa habari zaidi