Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kauli ya WHO kuhusu matibabu ya Figo nchini Tanzania

GettyImages 493216259 565c75eb5f9b5835e474b7de Kauli ya WHO kuhusu matibabu ya Figo nchini Tanzania

Fri, 26 Nov 2021 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

SHIRIKA la Afya Duniani (WHO) limepongeza juhudi zinazofanywa na sekta ya afya Tanzania kuokoa maisha ya watu wenye magonjwa ya figo kwa kuongeza upatikanaji wa huduma hizo nchini. Pongezi hizo zilitolewa na Mkurugenzi Mkazi wa WHO nchini, Dk Tigest Ketsela Mengestu kwenye mkutano wa saba wa Chama cha Madaktari wa Figo Tanzania unaofanyika Dar es Salaam.

“Juhudi zinazoendelea za serikali na Chama cha Madaktari wa Figo zinaiweka Tanzania kuwa miongoni mwa mataifa barani Afrika yatakayoongeza idadi wa madaktari bingwa wa figo kwani bado wanahitajika sana,” alisema Dk Mengestu. Magonjwa ya figo yana athiri mtu mmoja katika kila watu 10 duniani, ambao ni zaidi ya watu milioni 700. Ugonjwa huo unakadiriwa kuwaathiri takribani asilimia 14 ya watu katika nchi Afrika zilizo Kusini mwa Sahara.

Tafiti zilizofanyika Tanzania zimebaini ugonjwa huo upo kwa asilimia saba hadi 15 katika jamii huku hali ikiwa mbaya zaidi mijini. Kwa mujibu wa utafiti wa kitaifa uliofanyika Tanzania mwaka 2012 kwa watu wenye umri wa miaka 25 hadi 69, visababishi vya magonjwa ya figo kama vile kisukari vilikuwapo kwa asilimia tisa ya Watanzania na pia mmoja katika kila watu wanne alikuwa na shinikizo la juu la damu.

Tanzania imetajwa kuwa ni mojawapo ya nchi za Afrika zinazoweza kutoa huduma ya kupandikiza figo ambayo inafanyika katika Hospitali ya Taifa Muhimbili na Hospitali ya Benjamini Mkapa. Tanzania imewekeza katika kupata wataalau wenye ujuzi unaohitajika kutibu matatizo ya figo. Mwaka 2012 wakati Chama cha Madaktari wa Figo kinaanzishwa kulikuwa na wataalamu mabingwa wanne lakini sasa wapo 31.

Kwa mujibu wa WHO, rasilimali za kupambana na magonjwa ya figo duniani ni chache na hazijagawanyika kwa usawa, ambapo katika nchi zilizoendelea kuna wastani wa madaktari bingwa wa figo 28.5 kwa watu milioni moja wakati kwenye nchi zinazoendelea watu milioni moja wana daktari bingwa wa figo 0.31.

Tanzania imeanzisha mafunzo ya wataalamu wa kutibu figo katika Chuo cha Sayansi ya Tiba cha Muhimbili ambacho pia hivi karibuni kilianzisha mafunzo ya stashahada ya juu ya wauguzi wanabobea kwenye matibabu ya figo. Kwenye hotuba ya ufunguzi wa mkutano huo, Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Dk Jakaya Kikwete alikitaka Chama cha Madaktari wa Figo na sekta ya afya kwa ujumla kuendelea kushirikiana kubadilishana ujuzi na madaktari wa figo kutoka nchi zilizopiga hatua katika teknolojia na utaalamu wa matibabu ya magonjwa hayo.

Alisema juhudi zinapaswa kufanyika kuhakikisha matibabu ya kusafisha figo yanafanyika kwa bei nafuu ili watu wengi zaidi waweze kuyamudu. Kwa sasa kila hudhurio la huduma ya kusafisha figo linagharimu kati ya Sh 250,000 hadi Sh 300,000 na mgonjwa anahitaji kufanya huduma hiyo mara tatu kwa wiki.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live