Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kampuni ya SC Johnson kuisaidia Tanzania mapambano dhidi ya Malaria

Sc J Rais Samia akiwa kiwandani hapo

Wed, 20 Apr 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Rais wa Jamhuri ya Tanzania Samia Suluhu Hassan 19 Aprili,2022 ametembelea Kampuni ya SC Johnson (SC Johnson Institute of Insectice Science for Public Health) inayojishughulisha na Utafiti wa Wadudu Dhurifu waenezao Magonjwa katika Mji wa Racine ulioko jimbo la Wisconsin nchini Marekani na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mtendaji na Mwenyekiti wa Kampuni hiyo Dkt.Fisk Johnson.

Katika mazungumzo hayo, Rais Samia alieleza kuwa Malaria bado ni changamoto nchini Tanzania na kuwa asilimia 94 ya Watanzania wapo katika hatari ya kupata maambukizi katika kipindi cha mwaka nzima.

Aidha, Rais Samia alieleza jitihada mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na wadau ikiwemo kugawa vyandarua bure kwa wajawazito na watoto wa umri ya chini ya miaka 5, kupuliza dawa ukoko ya kuuwa mbu katika Halmashauri zenye kiwango kikubwa cha maambukizi ya Malaria, kutoa huduma za uchunguzi na matibabu pamoja na kufanya tafiti na ufuatiliaji wa mbu na wagonjwa wa Malaria.

Hata hivyo Rais Samia alieleza kuwa bado wananchi wa maeneo mbalimbali nchini Tanzania wanakosa huduma za uchunguzi na Matibabu ya Malaria kutokana na kukosekana kwa vituo vya kutoa huduma za Afya pamoja na uchache wa rasilimali za kugharamia mapambano dhidi ya Malaria.

Akiongea katika mazungumzo hayo, Mwenyekiti na Mkurugenzi Mtendaji wa SC Johnson Dkt. Fisk Johnson alieleza kuwa lengo kuu la kampuni hiyo ni kuboresha maisha ya watu.

Kampuni hiyo ya kifamilia iliyoanzishwa zaidi ya miaka 100 iliyopita imekubali kusaidia Tanzania katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Malaria katika maeneo mbalimbali ikiwemo kusaidia ujenzi wa vituo vya msingi vya kutoa huduma za afya (Zahanati) katika Mikoa yenye kiwango kikubwa cha maambukizi ya Malaria.

Vilevile, wameahidi kusaidia kuboresha miundombinu katika chuo cha udhibiti wa wadudu dhurifu waenezao magonjwa kilichopo Muheza, Mkoani Tanga (Muheza Vector control training centre) pamoja na kusaidia uboreshaji wa miundombinu kwa kushirikiana Utaalamu na Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) pamoja na Taasisi ya Afya ya Ifakara.

Katika ziara hiyo Mhe.Samia alipata kutembelea kiwanda cha Kampuni hiyo.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live