Dar es Salaam. Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) imetumia Sh777milioni kuwawekea vifaa vya usikivu watoto 21.
Akizungumza leo Jumapili Desemba 16, 2018 wakati wa kuwasha rasmi vifaa vya usikivu kwa watoto tisa, daktari bingwa wa masikio, kinywa na koo, Edwin Liyombo amesema Serikali ingetumia zaidi ya Sh2.1 bilioni iwapo wangepelekwa nje ya nchi.
“Tumefanikiwa kuokoa Sh1.3 bilioni kwa kutoa huduma hii ndani ya nchi haya ni mafanikio makubwa. Mwaka 2003 hadi 2016 walipelekwa watoto 50 lakini kwa kipindi cha miezi 15 pekee tangu mashine hii kuwekwa tumehudumia watoto 21,” amesema Dk Liyombo.
Mmoja kati ya wazazi ambao watoto wao wamewashiwa vifaa vya usikivu leo, Baraka Mukama amesema amefurahi kuona mtoto wake ameanza kusikia sauti na kuwa kama watoto wengine.
“Niligundua kuwa mwanangu hana uwezo wa kusikia alipofikisha umri wa miaka mitatu, tulikwenda hospitali na baada ya vipimo tukagundua kuwa hana uwezo wa kusikia, ila tunashukuru ameweza kufanyiwa upasuaji na sasa anasikia,” amesema Baraka ambaye ni mzazi wa Eliada.